in , ,

Ni miaka kumi sasa, tangu Marc Vivien Foe atutoke..

Miaka kumi iliyopita tarehe 26 ya mwezi wa sita, familia ya soka duniani ilimpoteza moja kati ya viungo bora kabisa kuwahi kutokea hasa barani Afrika.

Akiwa na urefu wa futi sita nukta mbili, mwenye umbo la miraba ya wastani, mweusi, Kijana aliyetokea kwenye familia masikini kwenye kijiji kimoja nje ya mji wa Younde kwenye kijiji cha Nkolo nchini Cameroon, mwaka 1975.

Anaitwa Marc Vivien Foe alipewa tuzo ya kamanda wa taifa la Cameroon,aliyefia vitani.

Foe alizaliwa mwaka tarehe mosi ya mwezi wa tano mwaka 1975 Younde Cameroon. Alianza soka akiwa na klabu ya daraja la pili ya Union Garoua kabla hajahamia kwenye klabu ya Canon Yaoundé, moja ya timu kubwa nchini Cameroon alishinda mataji kadhaa.

Nyota ya Foe ilianza kung`aa tangu alipoitwa kwa mara ya kwanza kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Cameroon mwaka 1993 na kisha aliongeza umaarufu wake na kuwafanya wakala na makocha wa vilabu kadhaa barani Ulaya kuanza kuitafuta saini yake mwaka 1994 kwenye fainali za kombe la dunia kule nchini Marekani.

Sir Alex Ferguson aliyekuwa kocha wa Manchester United mwaka 1998 aliwahi kwenda kufanya mazungumzo maalumu na wakala wa Foe na kisha kuonana na Foe mwenyewe lakini juhudi za kutaka kumsajili Foe zilishindikana baada ya kuvunjika mguu wakati akifanya maazoezi na timu yake ya taifa kwenye fainali za kombe la dunia nchini Ufaransa.

Licha ya kuvunjika miguu, bado Fergie aliwaambia viongozi wa United kuwa angelipenda kumsajili Foe lakini dili hilo lilishindikana na Foe alienda West United baada ya kupona majeraha yake kwa uhamisho ulioweka rekodi kwenye klabu hiyo ya mashariki mwa jiji la London kwa Pound milioni 4.2 kwa wakati huo.

Foe alihamia West Ham akitokea Lens ya Ufaransa alikodumu kwa miaka minne. Pamoja na kusajiliwa kwa uhamisho mkubwa kwenda Uptorn Park, Foe hakuwa na msimu mzuri chini ya kocha Harry Redknapp kwani baada ya msimu mmoja na nusu alirejea ufaransa na kujiunga na timu ya Olympique Lyonnais au Lyon kama inavyofupishwa ambako alidumu kwa misimu miwili kabla ya Kevlvin Keegan kocha wa wakati huo wa Manchester City hajaamua kumsajili na kumfanya mchezaji muhimu kwenye kikosi cha kwanza cha Man City.

Akiwa Man City Foe huenda Mungu ndo alikuwa akiionyesha dunia kilivyo kipaji cha Marc Vivien Foe mtu anatejwa kuwa na moyo wa huruma na wa kipekee, Alianza msimu vizuri na kufanikiwa kufunga magoli mengi na muhimu kwenye mechi ngumu.

Moja ya vitu ambavyo Mashabiki wa Man City hawatoweza kuvisahau ni goli lake la mwisho kwenye uwanja wa Maine Road maarufu kama Wembley ya Kaskazini, uwanja wa zamani wa Manchester City kabla ya hawajahamia kwenye uwanja wa City of Manchester au Etihad.

Foe alifunga bao hilo kwenye mechi dhidi Sunderland ambapo City walishinda 3-0.

Kifo cha Marc Vivien Foe kiliishitusha dunia ya wapenda kandanda, kwani ilikuwa ni ghafla sana. Ilikuwa ni kwenye michuano ya kombe la mabara kama hii inayoendelea nchini Brazil hivi sasa, hatua ya nusu fainali wakati Cameroon wakicheza na Colombia dakika ya 72, Foe alidondoka katikati ya uwanja na juhudi za kwenda kuokoa maisha yake zilifanyika kwa zaidi ya dakika 40 lakini zilishindikana.

Mashabiki wa soka, wachezaji na kila mkereketwa wa mpira wa miguu duniani alituma na salamu za rambirambi kwa namna ya kipekee. Thiery Henry nahodha wa wakati huo wa Ufaransa alishangilia goli lake kwenye mechi ya pili ya nusu fainali ya michuano hiyo kwa kuonyesha vidole juu kama ishara ya kumkumbuka Foe, ambapo kabla ya mchezo huo wachezaji wengi walitokwa na machozi kwa kumpoteza Foe.

Wachezaji wa Cameroon walioingia fainali ya michuano hiyo, walicheza wakiwa na majonzi kwenye mechi ya fainali, Nahodha Ligobert Song na Samwel Eto`o waliongoza timu hiyo kwa kubeba picha ya Foe na kusimama kwa dakika moja uwanjani kuomboleza.

Marc Vivien Foe alifariki kwa kile ambacho madaktari wanakitaja kama mshituko wa moyo. Nchini Cameroon Foe alipewa mazishi ya kitaifa na heshima zote, ambapo Serikali ilisimamia gharama zote.

Manchester City ilitenga eneo maalumu kama bustani kwenye uwanja wao zamani wa Maine Road kama ishara ya kumkumbuka Foe na kutangaza kutoitumia jezi namba 23 ambayo Foe alikuwa akiivaa klabuni hapo, kitendo ambacho kinaendelezwa hadi leo.

Lyon waliiweka jezi yake namba 17 kwa muda miaka kadhaa bila kuitumia lakini, baadaye jezi hiyo ilikuja kupewa kiungo wa timu ya taifa ya Cameroon Jean II Makoun.

Ni miaka kumi sasa tangu Foe aondoke duniani, akiwa ameacha mjane binti mdogo wa wakati huo Marie-Louise ambaye aliachiwa jukumu la kulea watoto watatu peke yake, wawili wakiume na binti mdogo ambaye baba yake aliondoka duniani akimuacha akiwa na miezi na miwili.

Swali kubwa ambalo limekuwa likiendelea kuulizwa hata nchini Cameroon ambako Foe alikuwa akitoa mchango mkubwa hasa kijijini kwake kwa kusaidia kusomesha vijana, kusaidia wazee, kutoa misaada kwa watoto yatima ni namna ambavyo familia yake imetunzwa na ilinufaika baada ya kifo chake.

Inaelezwa Manchester City ilikuwa na mkataba wa mkopo na Foe, lakini Olympique Lyon ilishindwa kuilipa familia ya marehemu fedha zilizosalia kwenye mkataba wake, jambo ambalo ukweli wake haujulikani mpaka leo.

Samwel Eto`o alijitolea kuilea familia ya Foe huku akitoa tuzo na fedha za zawadi zake mara kadhaa kwenda kwa familia ya Foe na watoto wake.

Shirikisho la kandanda duniani FIFA, limekuwa karibu na familia ya Foe ambapo mwaka 2009 kwenye mechi ya fainali ya kombe la shirikisho mwana wa kiume wa Foe ambaye alikuwa na miaka 14 alitoa hotuba fupi kuhusu kumbukumbu ya kifo cha baba yake.

Nchini Ufaransa kuna mfuko maalumu wa kusaidia watu wenye matatizo ya moyo kwa kumbukumbu ya Foe, ambapo mjane wa Foe Marie-Louise ndiye mlezi wa mfuko huo.

Licha ya kuondoka duniani miaka 10 iliyopita, Bado dunia hasa bara la Afrika linaendelea kukumbuka kifo cha Marc Vivien Foe hasa umuhimu wake kwa timu ya Cameroon ambayo ilikuwa imesheeni nyota wengi waliopa mafanikio makubwa timu hiyo tofauti na ilivyo sasa ambapo Cameroon imekuwa timu ya kawaida kwenye soka la Afrika na dunia ambapo hata kwenye viwango vya FIFA imepitwa kwa ubora na timu ya taifa ya Tahiti.

Mashabiki wa Manchester City walisema “A Lion Never Die, He Just Lays There Sleeping” Kwa maana Simba huwa hafi, analala tu chini kupumzika.

Mungu aiweke Roho ya Marc Vivien Foe mahala panapo Stahili, Ameen.

Enhanced by Zemanta

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Makocha ulaya hamahama

Igeni Ulaya katika kufanya usajili-Tenga