in , , ,

Manchester United mapambano

 

*Ni kumbakisha De Gea, kumpata Depay

*Sturridge na wakala wa Toure matatizo

 

Manchester United wanapambana kuhakikisha wanambakisha golikipa wao namba moja, David De Gea anayetakiwa na Real Madrid.

 

United wapo tayari kumshawishi kipa huyo Mhispania abaki kwa kumpa mshahara wa pauni 200,000 kwa wiki ili akubali kubaki Old Trafford.

 

Kuna tetesi kwamba De Gea ameshazungumza na Real juu ya kuhamia kwao kiangazi hiki na kilichobaki ni klabu mbili hizo kujadiliana.

 

Habari nyingine zinasema kwamba Man U wanakaribia kufikia mwafaka kumsajili kiungo wa Borussia Dortmund, Ikay Gundogan (24) kwa pauni milioni 20.5.

 

Kwa upande mwingine, klabu hiyo imepata pigo baada ya Liverpool kuelekea kuwazidi kete baada ya kuruhusiwa kujadiliana na mshambuliaji wanayemuwania kutoka PSV Eindhoven, Memphis Depay.

 

Depay (21) alitua kwenye Uwanja wa Ndege wa Manchester Alhamisi hii kwa ajili ya mazungumzo na Liver wanaohangaika bila mafanikio hadi sasa kuziba pengo la Luis Suarez waliyemuuza Barcelona msimu uliopita.

 

Man U waliwasiliana na PSV pia juu ya mchezaji huyo lakini walikuwa bado hawajapewa kibali cha kuzungumza naye, hivyo Liver wapo katika nafasi nzuri ya kumpata ikiwa watakubaliana maslahi.

 

Wakati United wakijiandaa kuvaana na Everton wikiendi hii, mchezaji wa Everton, Phil Jagielka anaamini nahodha wa United, Wayne Rooney bado atapatwa kigugumizi.

 

Jagielka anasema kwamba kila akirudi kwenye klabu yake hiyo ya zamani hushindwa kucheza vyema kutokana na mapenzi yake kwayo.

Bosi wa Liverpool, Brendan Rodgers ameonesha shaka juu ya mshambuliaji wake, Daniel Sturridge juu ya utimamu endelevu wa mwili wake.

 

Kwa sababu hiyo, Rodgers anasema kwamba itabidi klabu itafute mpachika mabao wa kuaminika atakayeisaidia timu kwa kucheza kila wiki kwa kiwango cha juu.

 

Kocha wa Southampton, Ronald Koeman anayetakiwa na Timu ya Taifa ya Uholanzi kuchukua nafasi ya Guus Hiddink amesema haondoki Saints ng’o.

 

Koeman amesema hakuna timu wala klabu itakayoweza kumshawishi aondoke hapo kabla mkataba wake haujamalizika.

 

Amesema hata Barcelona, klabu aliyochezea na kuzoa nayo ubingwa mara nne wa La Liga haiwezi kumbadili fikra zake, na amewataka wachezaji wake watulie na kuchapa kazi.

 

Kiungo wa Queen Park Rangers (QPR), Joey Burton amesema wakifanya kazi kwa kujituma kama timu wanaweza kuepuka kushuka daraja, lakini akasema kwa sasa ndio timu mbovu zaidi katika ligi kuu ya England.

 

Kocha wa timu ya daraja la pili ya Derby, Steve McClaren amekiri kwa mara ya kwanza kwamba maofisa wa Newcastle walimfuata ili akawe kocha huko.

 

Newcastle wapo katika wakati mgumu kwenye ligi, chini ya kocha wa muda, John Carver baada ya kocha wao Alan Pardew kuondoka na kujiunga na Crystal Palace ambao sasa wanafanya vyema kwenye ligi.

 

Washabiki wa Newcastle wanaendesha harakati dhidi ya mmiliki wa klabu hiyo, Mike Ashley kutokana na mwenendo mbaya wa timu na wanaamini hajajituma vya kutosha kwenye usajili na kupata kocha mahiri.

 

Kiungo wa zamani wa Arsenal, Ray Parlour amemshauri kocha Arsene Wenger kumfanya kipa wa Chelsea, Petr Cech (32) kipaumbele kwenye usajili wa kiangazi unaokaribia.

 

Kocha wa Manchester City, Manuel Pellegrini amesema kwamba wakala wa kiungo wao hodari, Yaya Toure aitwaye Dimitri Seluk ametokea kuwa tatizo kwa klabu hiyo.

 

Seluk mara kadhaa amekuwa akiwashutumu City akisema hawamtendei vyema Toure, kama kumnyima salamu na zawadi siku yake ya kuzaliwa mwaka jana na pia kutompa heshima inayostahili.

 

Majuzi Seluk alisema anataka kuzungumza na City kwa sababu amepata dili kadhaa nzuri kutoka klabu nyingine kwa ajili ya kumsajili mchezaji huyo. Pellegrini amedai Toure anapenda kubaki Etihad.

 

Hata hivyo, majuzi Toure alikaririwa akisema kwamba hawezi kukaa mahali ambako inaelekea ama hapendwi au hatakiwi. Amekuwa akilaumiwa na maofisa wa City kwa kucheza chini ya kiwango na kuwa sababu yao kushindwa kutetea vilivyo ubingwa unaoelekea Chelsea.

 

Tottenham Hotspur watatakiwa kumlipa mshambuliaji wao aliyegeuka garasa, Emmanuel Adebayor, walau pauni milioni 2.5 ili kumwondosha klabuni hapo kiangazi hiki.

 

Adebayor (31) yupo huru kuondoka lakini ameapa kwamba haendi kokote kwa sababu bado ana mkataba wa mwaka mzima na analipwa pauni 100,000 kwa wiki huku akiwa hana chochote anachoisaidia klabu.

 

Kiungo wa Everton, Gareth Barry amemshauri mchezaji mwenzake aliye pia Timu ya Taifa ya England, Ross Barkley (21) kukataa ofa kutoka Manchester United au klabu yoyote kiangazi hiki na abaki na Toffees.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Wenger atamlipua Mourinho?

Arsenal, Chelsea nguvu sawa