in ,

Man City imekaribia kuwa bingwa…

LIGI Kuu ya Uingereza inaelekea ukingoni, huku Manchester City ikiukaribia ubingwa huo kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 44. Ushindi wa Jumapili iliyopita wa vijana hao wa Roberto Mancini ugenini dhidi ya timu ngumu ya Newcastle United umeisogeza pazuri. Magoli mawili safi ya Yaya Toure yamemlainisha Mancini ambaye siku zote, hata baada ya kuwa na uwiano mzuri wa magoli dhidi ya United, amekuwa akisema bado mahasimu wao hao ndio wenye nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa. Kinachosubiriwa kwa hamu ni michezo ya mwisho Jumapili ijayo kati ya Manchester City watakaokuwa nyumbani Etihad kukipiga na Queen Park Rangers (QPR) wakati Manchester United wakimenyana na Sunderland kwenye uwanja wa Loftus Road. Adui yako mwombee njaa, na Bosi wa Manchester United, Sir Alex Ferguson ameweka matumaini yake mikononi mwa Kocha Mkuu wa QPR, Mark Hughes aliyepata kuwa mshambuliaji wa United na pia kocha wa City.

Katika kile kinachoweza kuwa kama kichekesho, Ferguson anasema anatamani Hughes mwenyewe angekuwa anacheza katika mchezo huo muhimu pia kwa QPR wanaojaribu kujinasua kushuka daraja. “Hatima yote ya klabu hii (Manchester United) yaweza kuwa kwenye mchezo huo, na ningetamani Sparky (Hughes) angekuwa anacheza. Mark anaijua kazi yake vyema. Alifukuzwa na City bila kuzingatia maadili na atakumbuka hilo,” anasema Ferguson. Hughes mwenyewe anasema ingekuwa safi sana ikiwa wangekwenda Etihad na kupata pointi, kwa sababu City wanawania kombe na timu yake inang’ang’ania kubaki kwenye ligi kuu. “Nadhani nilitazama ratiba hii nilipoanza kazi hii na nikaona kuna kitu kigumu kinakja – lakini sasa ni juu yetu wenyewe, bado tunayo fursa ya kuhakikikisha tunabaki kwenye ligi hii kwa jitihada zetu wenyewe,” anasema Hughes. Bosi wa City, Mancini aliyetabasamu baada ya ushindi dhidi ya Newcastle kwenye mchezo mgumu ambao mabao yalipatikana kipindi cha pili, anaonyesha amejawa matumaini. Mfungaji wa mabao hayo, Yaya Toure aliyeonekana kuzungumza kwa faragha na Mancini kabla tu ya kuanza mechi hiyo muhimu, anasema lazima wajiimarishe na kwa vile wapo nyumbani, watapata nguvu ya washabiki wao. Mancini alimwambia Toure, kwa mujibu wa mchezaji huyo mwenyewe, lazima aweke bidii ya kipekee na kuzaa matunda (mabao) kwa sababu ni mchezaji muhimu, na baada ya kosa kosa nyingi, alipata mabao muhimu. Ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Swansea ilioupata United Jumapili haukupokewa kwa furaha kubwa, kwa sababu ulichofanya ni kurejesha msimamo uliokuwa awali – City wakiwa juu kwa tofauti ya mabao manane. Ikiwa timu zote hizo za jijini Manchester zitashinda Jumapili, nani ataweza kufuta pengo hilo? Hakuna kisichowezekana, japokuwa inahitajika kazi ya ziada kwa mazingira ya sasa. Itakumbukwa kwamba Manchester United ilipata kufanya maangamizi kwenye ligi kwa kuzifunga Wolverhampton Wanderers mabao 10–1 Oktoba 15, 1892. Kadhalika iliinyuka Walsall 9-0 Aprili 3, 1895 kabla ya kurudia kipigo kama hicho kwa Darwen Desemba 24, 1898 na dhidi ya Ipswich Town kwenye Ligi Kuu Machi 4, 1995. Haijasahaulika bado, bila shaka, jinsi ilivyoichapa Arsenal mabao 8-2 Jumapili ile ya Aprili 28 mwaka jana, lakini leo hii itaweza kufunga idadi hiyo? United ikiweza, kipi kitaizuia City nao kufanya karamu kama hiyo au zaidi kwa kasi waliyo nayo? Nahodha Mbelgiji wa Man City, Vincent Kompany alikuwa na haya ya kusema kuhusu timu yake baada ya ushindi wa Jumapili: “Ufanisi wa ajabu kwa timu hii. Ninayo furaha kubwa na najivunia ninapotoka uwanjani nikiwa na wachezaji hawa maarufu.” Kwa majirani wao wa United, wote wakiitana ‘jirani mwenye kelele’, Rio Ferdinand aliyetoka mapema kwenye mechi dhidi ya Swansea alisema; “sasa mpaka mechi ya mwisho wa msimu ndipo iamuliwe ubingwa unakwenda wapi…mambo yanaendelea mpaka mwishoni mwa wiki ijayo!” “Tulipania kushinda mechi hii iwe iwavyo na tulifanikiwa kufanya hivyo dimbani,” ni maneno ya Sergio Aguero wa City ambaye Jumapili alikuwa na kigugumizi akiwa ndani au karibu na eneo la 18. Je, kiu ya ubingwa kwa miaka 44 itatulizwa Jumapili ijayo au United itaibuka na ngekewa na kuchukua kombe? Wakichukua City, Ferguson ameshasema kitakachokuwa kimesababisha ni uzembe wao (United) kwenye mechi dhidi ya Everton walipokubali kudhibitiwa dakika za mwisho na kutoka sare ya mabao 4-4. Pamoja na kupata faraja kwa kufuta tofauti ya pointi nane iliyokuwepo kati ya City na United wiki chache zilizopita, Mancini anasema kikubwa ni kunyakua pointi tatu Jumapili. “Mambo bado, ni muhimu kupata pointi tatu wiki ijayo. Tumefanya jitihada kubwa – bado kuna mchezo mmoja. QPR ni wagumu, wanapambana kuepuka kushuka daraja. Hakuna kilichobadilika, ni ama kupata au kukosa, hakuna kutegemea timu nyingine tena,” anasema Mtaliano huyo. Man City iliongoza ligi kwa tofauti kubwa ya pointi kwa muda mrefu, kabla ya kuka kupoteza mwelekeo na kuifanya United ipande taratibu hadi kuifikia na kisha kuivuka kwa point inane. Wakati wa masahibu hayo, City walikuwa na sintofahamu ya mchezaji wao muhimu wa Kiargentina, Carlos Tevez aliyekuwa amekosana na kocha wake baada ya kudaiwa kukataa kupasha ili aingie dimbani kucheza dhidi ya Bayern Munich Septemba 27, 2011. Baada ya hao Teves alikosa mechi nyingi na hata kuondoka kambini na kwenda kwao Argentina bila ruhusa, kabla ya kurejea na kupatiwa adhabu, ikiwamo faini. City ilikuwa pia na mkasa wa mshambuliaji wake Mtaliano, Mario Balotelli ambaye amekuwa na vitendo vya utovu wa nidhamu na wakati mwingine vituko vya mara kwa mara. Tangu amalize kutumikia adhabu ya kadi nyekundu aliyopata kwenye mechi ya ligi dhidi ya Arsenal Aprili 8, 2012, Balotelli hajacheza tena. Safu ya ushambuliaji inaonekana kuwa tishio wanaposhirikiana Tevez na Aguero, japokuwa Jumapili Tevez hakufurukuta na alitoka akaingia Edin Dzeko. Kana kwamba ni yale ya sizitaki mbichi hizi za Sungura, Sir Ferguson alikuwa na hili wakati ligi ikielekea ukingoni: “Tumeshatwaa kombe hili mara kadhaa kwa hiyo hata tukilikosa sijali sana, City wanapewa nafasi kubwa sana na watafanya kila wawezalo kulichukua. Matarajio na wajibu wa wachezaji wa Manchester United ni kushinda mechi. Tutakwenda pale tukiwa na matumaini. Haitakuwa rahisi lakini itabidi.” Wakati Ligi Kuu ikitimiza miaka 20, mfalme wa soka atatangazwa kwenye mechi muhimu mbili za mwisho, ambapo mechi zote za Jumapili zitaanza saa 9.00 kwa saa za Uingereza.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Man City imejisafishia njia ya ubingwa?

TAVA Yawanoa Makocha wa Wavu Mikoani