in

Vilabu vya Tanzania na Usajili….

MPAKA msimu mpya wa ligi kuu ya Tanzania Bara unakaribia kuanza Simba ndiyo inaweza kuwa timu iliyoingiza fedha nyingi zaidi kutokana na biashara ya kuuza wachezaji nje ya nchi.

Lakini kwa biashara ya kuuza wachezaji ndani ya Tanzania basi tuzo hii kama ingekuwepo ingestahili kwenda kwa klabu ya Mtibwa sugar yenye masikani yake Manungu, Turiani mkoa wa Morogoro.

Klabu hii ya Turiani kwa zaidi ya miaka kumi sasa imekuwa ikiongoza kwa kuuza wachezaji wenye viwango bora kwa timu za hapa hapa nyumbani, hasa kwa klabu kubwa za Simba na Yanga, ambazo haziachi kuiandama klabu hiyo kila kipindi cha usajili kinapofika.

Kwa mfano msimu huu tayari wakata miwa hao wa Turiani imewauza wachezaji wake Shaabani Kadoambaye ni mlinda mlango wake chaguo la kwanza na winga machachari mwenye kasi Jullius Mrope kwa klabu bingwa ya soka nchini Yanga.

Huku mlinzi wake tegemeo Obadia Mungusa na kiungo mchezeshaji Salumu Machaku wakiishia mikononi mwa wekundu wa msimbazi, Simba.Kwa soko la wachezaji la Tanzania kiwango cha juu kabisa kusajiliwa mchezaji hasa akitokea timu kama Mtibwa Sugar inakadiriwa kufikia kwenye shilingi milioni 30 na cha chini ni shilingi milioni 15 hivi.

Tuchukulie kwa mfano wachezaji wote hao wameuzwa kwa shilingi milioni 20 kila mmoja, basi wakata miwa hao watakuwa wamepata shilingi milioni 80, kwa timu ambayo kwa kawaida yake huchukua wachezaji chipukizi na kuwakuza na baadaye kuwauza kwa gharama kubwa kabisa.

Katika msimu wa mwaka 2009/10 Mtibwa ilimuuza kiungo wake mkabaji aliyekuwa katika kiwango cha juu kipindi hicho Abdulhalim Humudu kwa Simba kwa makadirio ya shilingi za kitanzania zaidi ya milioni 20 na nyuma ya msimu huo pia ilimuuza kiungo mshambuliaji wake Uhuru Selemani kwa kiwango kama hicho.

Timu yenye sera nzuri za kuendeleza na kuuza wachezaji, kwa sababu mchezaji kama Salumu Machaku alifungiwa virago na klabu ya Azam katika msimu wa mwaka 2009/10 lakini Mtibwa Sugar ikamchukua na leo hii inatengeza kiwango hicho cha fedha.

Kadhalika kwa winga Jullius Mrope alishaanza kupotea kwenye ramani ya soka lakini Mtibwa ikamsajili akitokea Moro United ambayo ilishuka daraja. Hapa ni wazi katika hali kama hii Mtibwa itakuwa imempata kwa bei nafuu lakini ikaja ikamuuza bei nzuri katika klabu ya Yanga.

Katika kipindi cha kati ya miaka mitano mpaka sita iliyopita Mtibwa imewauza wachezaji kama vile Amir Maftah,Abdi Kassim na Kigi Makasy kwa bei nzuri kwenda klabu ya Yanga. Wakati nyuma zaidi iliwauza Mussa Mgosi na beki Victor Costa kwenda timu ya Simba.
Ukiangalia mifano hiyo sera ya kuuza na kukuza wachezaji ya klabu ya Mtibwa Sugar inajipambanua wazi kabisa, kwani kila mwaka inafanya vizuri katika soko la kuuza wachezaji ukilinganisha na timu nyingine.

Na ubora wa sera zao za kukuza na kuendeleza wachezaji nalo huko wazi kabisa kwani yenyewe ndiyo klabu inayochukua wachezaji chipukizi na kuwaendeleza, hapa nakumbuka ilivyomchukua kiungo wa kimataifa wa Tanzania Nizar Khalfani kutoka timu ya taifa ya chini ya miaka 17 Serengeti Boys mwaka 2005 na baadaye kumuuza Kuwait katika klabu ya Al Tadhamon.

Wakati Mtibwa ikifanya vizuri katika soko la kuuza wachezaji nyumbani Simba imekuwa ikifanya vizuri katika soko la kimataifa kwa kuuza wachezaji wake Ulaya, Asia na katika nchi za Afrika.

Tukirudi nyuma zaidi kwenye miaka ya 2000 Simba ilimuuza nahodha wake Selemani Matola katika klabu ya Supersport ya Afrika Kusini kabla ya baadaye kumuuza mlinzi wake wa kati Victor Costa huko huko Afrika Kusini.

Mwaka 2007 Simba ikamuuza mshambuliaji wake Danny Mrwanda katika klabu ya Al Thadhamon ya nchini Kuwait mara baada ya kuonekana na klabu hiyo kufuatia ziara ya mwezi mmoja ya timu ya taifa katika nchi za Denmark na Uswisi.

Msimu wa 2008 Simba ilimuuza kiungo mkabaji wake Henry Joseph katika klabu ya Konsivinger ya nchini Norway, sambamba na kiungowa ushambuliaji kutoka Nigeria Emmeh Ezechukwu.

Baadaye Dan Mrwanda akarudi kuchezea Simba  kwa muda kabla ya kumuuza tena, safari hii aliuzwa katika klabu ya Dt Long An ya Vitenam. Simba pia ilivuna hela nyingi kwa kumuuza kiungo mchezeshaji wake Haruna Moshi Boban katika klabu inayoshiriki ligi kuu ya Sweden ya Gefle Fc. Sasa Haruna amerudi kuichezea tena Simba baada ya kuvunja mkataba na klabu hiyo ya Sweden.

Mwaka huu klabu hiyo ya Msimbazi imewauza washambuliaji wake Mbwana Samatta na Patrick Ochan  kwa mabingwa wa Afrika TP Mazembe ya Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo. Inasemekana kwamba Simba imeingiza zaidi ya shilingi milioni 300 kwa mauzo ya wachezaji hao.

Unachoweza kuona hapa ni kwamba hela waliyotumia katika kuwasajili wachezaji hao imeudi kwani ilimsajili chipukizi Mbwana Samatta kwa karibu shilingi milioni 20 hivi toka African Lyon, sina hakika na kiwango walichotumia katika kumsajili mganda Patrick Ochan kutoka St. George lakini haiwezi kuzidi shilingi milioni 40.

Hakuna unachoweza kusema hapo zaidi ya biashara nzuri wekundu hao wanaifanya kupitia mauzo ya wachezaji wake. Hali ikiwa hivyo kwa Simba kwa wapinzani wao wakuu Yanga ni tofauti kabisa yenyewe imeuza wachezaji watatu tu, wawili nje ya na mmoja hapa hapa Tanzania.
Katika msimu wa mwaka 2007 kama sitakosea Yanga ilimuuza winga wake wa kulia Saidi Maulidi katika klabu ya Onze Bravo inayoshiriki ligi kuu nchini Angola kwa takribani shilingi milioni 50 hivi za kitanzania, kwa umri wa Saidi Maulidi ni wazi hiyo ilikuwa biashara nzuri kwa sababu umri wake ulishamtupa mkono.

Mwaka 2009/10 ikamuuza mchezaji anayekadiriwa kuwa na uwezo wa juu kuliko wote nchini kwa sasa Mrisho Ngassa kwa shilingi milioni 58 za kitanzania katika klabu ya Azam Fc.

Ikumbukwe kwamba kabla ya kusajiliwa na Azam Ngassa alikuwa anatakiwa na klabu ya Lov Ham inayoshiriki ligi daraja la kwanza nchini Norway, tena bila ya majaribio lakini uongozi wa Yanga chini ya mwenyekiti wake Imani madega ulikataa kumuuza kwa madai kwamba dola elfu 50 ambazo Lov Ham walikuwa tayari kutoa zilikuwa ndogo kulinganisha na thamani ya mchezaji mwenyewe.

Baadaye Ngassa akapata nafasi ya kufanya majaribio katika klabu ya West Ham chini ya meneja wake kipindi hicho Gianfranco Zola, majaribio ambayo hata hivyo alishindwa na hivyo kumlazimu kurudi nyumbani, ndipo kwa aibu Madega akamuuza Azam Fc kwa shilingi milioni 58.
Ilikuwa ni kwa aibu kwa sababu alikataa kumuuza katika klabu ya Lov Ham ya Norway kwa madai fedha zilikuwa ndogo kulinganisha na thamani ya mchezaji mwenyewe, lakini hakuangalia faida nyingine ambazo mchezaji, klabu na taifa ingepata kwa kumuuza Ngassa Norway.
Dola elfu 50 ni kubwa zaidi kwa kwa shilingi za kitanzania ni zaidi ya shilingi milioni 80, ambazo ni tofauti kabisa na shilingi milioni 58 ambazo Ngassa aliuzwa Azam. Pia Madega kama mwanasheria angetumia taaluma yake vizuri kipindi hicho kwa kuingiza kipengele ambacho kingeweka wazi kuwa kama Lov Ham itamuuza zaidi Ngassa basi nayo inufaike kwa asilimia kadhaa, kwa kumuibua na kukuza kipaji cha mchezaji huyo.

Ngassa wiki hii anacheza mechi ya kirafiki akiwa na timu ya Seattle Sounders ya Marekani ambayo itacheza na Manchester United ya Uingereza, yuko kwenye majaribio Marekani akicheza vizuri mechi hiyo ya kirafiki anaweza akasajiliwa na Seattle Sounders au hata Manchester United na kuandika historia mpya kwa wachezaji Tanzania, na akiuzwa faida kubwa itaenda kwa Azam sio Yanga ambayo imetumia muda mwingi kumuandaa.

Yanga tena kwa shinikizo la vyombo vya habari ikamuuza kiungo wake Abdi Kassim katika klabu ya Dt Long An ya nchini Vietnam, kwani naye walikuwa wanataka kukutaa kumuuza, kwa sababu ambazo hazina msingi.

Iliwahi kukataa kumuuza Jerry Tegete aliyefuzu majaribio katika klabu ya Dalkurd inayoshiriki ligi daraja la kwanza Sweden na pia kumuzuia kwenda kwenye majaribio nchini Sweden,  kipindi cha mwaka 200/910 kiungo wake Athmani Idd.

Yanga hauzi wachezaji nje, inatumia gharama kubwa za kusajili pengine kuliko timu yoyote hapa nchini lakini pia haifiki mbali kwenye michuano ya kimataifa, kitu ambacho labda kingeweza kuwafanya waeleweke kwanini hawauzi wachezaji nje ya nchi.
Shirikikisho la soka nchini, TFF inapaswa kuweka sheria itayoibana timu kama Yanga na nyinginezo ziweke sera za kuuza wachezaji wake hasa nje ya nchi kwa manufaa ya mchezaji mwenyewe, klabu, timu ya taifa na taifa kwa ujumla

— On Tue, 7/12/11, Israel Saria <[email protected]> wrote:

From: Israel Saria <[email protected]>
Subject: Re: hiyo kaka
To: “Clecence Kunambi” <[email protected]>
Date: Tuesday, July 12, 2011, 5:17 AM

Ok.ngoja niipitie basi….thanks

Send from my Iphone

On 12 Jul 2011, at 13:06, Clecence Kunambi <[email protected]> wrote:

Na Clecence Kunambi
MICHUANO ya kombe la Kagame ilifikia tamati wiki hii kwa mabingwa wa soka Tanzania bara, Yanga kutangazwa wafalme wapya wa kombe hilo.

Yanga imefanikiwa kutwaa kombe hilo kwa kuwafunga wapinzani wao wakubwa Simba kwa bao 1-0 katika muda wa nyongeza, bao lililowekwa kimiani na mshambuliaji wao Kenneth Asamoah kutoka Ghana.

Mshambuliaji huyo kipenzi cha wanajangwani alizima ndoto za mabingwa hao wa kihistoria kuweka rekodi ya kutwaa kombe hilo kwa mara ya saba alipofunga bao kwa kichwa akiunganisha krosi nzuri ya kiungo mchezeshaji Rashid Gumbo.

Gumbo,  mchezaji mwenye kipaji cha pekee cha kumiliki mpira aliingia akitokea benchi katikati ya kipindi cha kwanza kuchukua nafasi ya kiungo mkabaji Juma Seif aliyeumia, aliambaambaa na mpira kwenye wingi ya kushoto akiwatoka wachezaji Mohamedi Banka na Saidi Cholo na baadaye kutoa krosi murua iliyounganishwa kiufundi na mshambuliaji huyo  wa zamani wa Fc Jagodina ya Serbia.

Mara ya mwisho Yanga kutwaa kombe hilo ilikuwa ni mwaka 1999 huko Kampala Uganda ilipoifunga Sports Club Villa ya nchini humo kwa mabao 4-5 kwa njia ya penati, ambapo matokeo katika muda wa dakika 90 yalikuwa ni 0-0 na hivyo kulazimu kwenda muda wa nyongeza.

Kwa ushindi huo Yanga imeandika historia mpya ya mashindano hayo, kwani ni kombe lake la nne ikiwa imewahi kutwaa kombe hilo kwenye miaka ya 1975 huko Zanzibar, mwaka 1993 na 1999 huko Kampala Uganda na mwaka huu katika ardhi ya nyumbani.

Katika michuano hii ya mwaka huu Tanzania iliwakilishwa na timu tatu ambapo ni mabingwa watetezi Simba kwa maana ya msimu uliopita, washindi wa pili Yanga na kwa upande wa Zanzibar walikilishwa na timu ngeni kabisa katika mashindano hayo, timu ya Ocean View.

Katika michuano hiyo ya wiki mbili hakukuwa na kipya sana kutoka kwa timu zetu kubwa za Simba na Yanga kwa maana ya ubora wa kiwango cha uwanjani na wachambuzi wa masuala ya soka wanasema kwamba uenyeji na uzoefu wa timu hizo katika mashindano hayo kwa kiwango kikubwa vilichangia timu hizo kufika hatua ya fainali.

Timu pekee kutoka Tanzania ambayo ilionyesha kiwango bora ni Ocean View ya Zanzibar ingawa uchanga wake katika michuano hiyo uliifanya itolewe katika hatua ya makundi, lakini ilicheza soka la kifundi na kitimu tofauti na Simba na Yanga.

Katika michuano hiyo ambapo Yanga na Simba zote zilikuwa katika kituo cha Dar es salaam kutokana na utashi wa Baraza la Vyama vya Soka kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati(CECAFA) na Shirikisho la Soka nchini, TFF zikiamini kuwa kuziweka kituo hicho kungetengeneza faida kubwa ya mapato kutokana na ukweli kwamba mkoa huo maarufu nchini ndio wenye washabiki wengi wa soka wa Simba na Yanga na wenye vipato vya kuingia mpirani.

Katika kituo hiki cha Dar es salaam Simba ilipangwa kundi A ikiwa na timu za Vitalo ya Burundi, Ocean View ya Zanzibar na Etincelles ya Rwanda.Simba ndio ilikuwa ya kwanza katika kundi hili ambalo halikuwa gumu, ingawa ilipata wakati mgumu ilipocheza na Vitalo na Red Sea kwani haikuweza kupata bao hata moja.

Yanga ndio ilikuwa kundi la kifo, kundi B lililokuwa na timu za El Merreikh ya Sudan, Bunamwaya ya Uganda na Elmani ya Somalia. Merreikh ndio ilionekana kama timu tajiri kwa kuwa wachezaji wake wengi ghali, ilicheza soka la kuvutia na la ufundi wa hali ya juu, katika mchezo wake wa kwanza dhidi ya Yanga zilitoka sare ya mabao 2-2.

Bunamwaya iliundwa na wachezaji wengi chipukizi ilimaliza ikiwa ya tatu katika kundi hilo na kupata kucheza hatua ya robo fainali kama timu iliyoshindwa kwa taabu, “Best Loser” sambamba na Yanga vinara wa kundi hilo na Merreikh walioshika nafasi ya pili.

Elman timu kutoka Somalia kama kawaida yake ingawa angalau ilijitahidi katika mashindano ya mwaka huu, hasa katika mchezo wao dhidi ya Yanga ambapo iliwabidi mpaka dakika za lala salama kuweza kupata mabao, katika ushindi wake wa mabao 2-0 dhidi ya timu hiyo.

Kituo cha Morogoro kilikuwa na timu za St.George, Ulinzi ya Kenya na APR ya Rwanda ambayo ndio ilikuwa bingwa mtetezi wa mashindano hayo na Ports ya Djibout.Lilikuwa kundi gumu kwa maana timu zote hizo zilikuwa na ubora wa hali ya juu ukiachilia mbali Ports ambayo ndio ilikuwa kapo la magoli.Wachunguzi wa mambo wanaamini hili ndilo lilikuwa kundi lenye timu ngumu na St George ndiyo ilikuwa timu bora kwa maana ya soka la kiufundi.

Katika hatua ya robo fainali Simba iliifunga timu ngumu ya Bunamwaya kwa mabao 2-1,Yanga ikaifunga Red Sea kwa penati 4-3,El Merreikh ikiitoa Ulinzi Kenya kwa penati na St George ikaifunga timu ya Vitalo ya Burundi na kutinga hatua ya nusu fainali.

Mpaka zinaingia fainali Simba na Yanga zote hazikuonyesha kandanda la kuvutia zaidi ya kucheza kwa uwezo wa mchezaji mmoja mmoja na kwa shinikizo la mashabiki wao zaidi kuliko muunganiko wao kama timu.

Makocha wa timu hizi mbili, Sam Timbe wa Yanga na Mosses Bassena wa Simba hakuna hata mmoja kati yao aliyewahi kukiri kuwa timu zao zilicheza vizuri zaidi ya kufurahia matokeo na kusema kwamba wanayatumia mashindano haya katika kutengeneza timu zao kwa ajili ya michuano kimataifa kama vile klabu bingwa Afrika na kombe la shirikisho.

Ukiachilia mbali ukweli wa kwamba timu zote hazikupata muda mzuri wa maandalizi kutokana na kwamba ndio ligi ilikuwa imekwisha na wachezaji kuwa mapumzikoni, kuchelewa kupatikana kwa mdhamini wa kuandaa mashindano hayo, kuliathiri kwa namna moja au nyingine maandalizi ya timu hizi, lakini kuna kitu kimejificha ndani ya timu hizo.

Hakika timu hizi zinaundwa na wachezaji wengi wapya kila msimu kitu ambacho hata zipewe muda gani, bado itakuwa ngumu kuweza kuwaunganisha, wakazoeana na kucheza pamoja kama timu, achilia mbali mabadiliko ya mara kwa mara ya makocha.
Uthibitisho ni vikosi vya timu hizo vilivyoshiriki mashindano haya vilikuwa na sura nyingi mpya kuliko zilivyokuwa msimu uliopita.

Wachezaji Rashidi Gumbo,Julius Mrope,Oscar Joshua, Kenneth Asamoah, Hamisi Kiiza, Godfrey Taita waliocheza karibu mechi zote za Yanga ni wapya na hivyo kufanya washindwe kuzoeana na kuleta radha ya soka safi.

Kadhalika wachezaji kama Dereck Walulya, Patrick Mafisango, Saidi Chollo, Haruna Moshi,Ulimboka Mwakingwe, Athumani Idd, Isihaka Rajabu na Mwinyi Kazimoto ni wageni katika kikosi cha Simba cha mwaka huu.

Hao wote ni wachezaji wanaoonekana kuwa ni wenye vipaji vya hali ya juu, lakini vipaji vyao havikuweza sana kuleta kandanda safi zaidi ya kila mmoja kuonyesha uwezo binafsi na sio muunganiko wao kama timu.

Mbali na kushindwa kuunganika kama timu lakini pia walionekana katika muda mwingi wa mashindano hasa mechi zilizokwenda mpaka muda wa nyongeza kukosa stamina na kuchoka haraka hali iliyotoa picha halisi ya kukosa mazoezi ya kutosha kama timu.

Kadhalika hakukuwa na ubunifu kwa wachezaji hao zaidi ya mashabiki wao kuucheza mpira kuliko wao wenyewe, kwa maana shinikizo la kelele pindi wachezaji hao wanapopata mpira, hawaachwi huru kufanya maamuzi binafsi.

Washabiki wakimwambia mchezaji fulani piga, naye hufanya hivyo muda huo huo, kitu kinachothibitisha kwamba ni mashabiki wanaoucheza mchezo kuliko wachezaji wenyewe na hii hufanya washindwe kuwa wabunifu na mwisho wa siku kushindwa kuonyesha uwezo wao na kuharibu radha nzima ya soka.

Ungependa kuangalia jinsi timu kama za El Merreikh, St. George au Bunamwaya zilivyokuwa zikicheza, zilicheza kitimu, kwa malengo kulingana na staili ya timu wanayokutana nayo, hali inayoonyesha kuwa walikuwa pamoja kama timu kwa muda mrefu.
Kwa kawaida ya mashindano mara nyingi vipaji vipya huweza kuvumbuliwa kupitia mashindano ambayo timu zao zinacheza, kwa mfano katika fainali za kombe la dunia zilizofanyika Ufaransa mwaka 1998 mchezaji Michael Owen aliweza kuvumbuliwa hasa alipofunga bao safi la ushindi katika mchezo wa robo fainali dhidi ya Argentina, Owen alikuwa na miaka 17 kipindi hicho.

Cha kusikitisha katika michuano ya mwaka huu ya kombe la Kagame ukiangalia ushiriki wa timu zetu hasa Simba na Yanga, hakuna chipukizi hata mmoja aliyepewa nafasi ya kuonyesha uwezo wake, sura nyingi zilizong,ara ni zile zile.

Hakuna jipya kwa wachezaji kama Haruna Moshi, Ulimboka Mwakingwe, Mohamedi Banka wa Simba wala Oscar Joshua, Juma Seif, Julius Mrope, Rashidi Gumbo, Nurdin Bakari kutoka Yanga kwani ni wachezaji ambao tayari uwezo wao unajulikana.

Yale yale kwa timu zetu kwa timu hizi kuendelea na tabia zao za kushindwa kuwa na sera nzuri za kuendeleza wachezaji chipukizi, zaidi ya kutaka ambao tayari wameshavumbuliwa.

Chipukizi kama Salum Telela, Omega Seme,David Luhende,Abuu Ubwa kutoka Yanga ambao wapo katika timu ya taifa ya chini ya miaka 23 majina yao hayakuorodheshwa katika wachezaji walioshiriki michuano hii, nini kukaa benchi.

Kadhalika Shomari Kapombe na Kelvin Chale kutoka Simba ambao nao wako katika timu ya taifa chini ya miaka 23 nao hawakupata nafasi ya kushiriki mashindano haya, kwani kama wenzao wa Yanga nao majina yao hayakuorodhezeshwa kwa ajili ya michuano hii.

Kinachoonekana hapa ni muendelezo wa tabia za wanachama, viongozi na makocha wa timu hizi kutaka matokeo na sifa binafsi zaidi na sio kuendeleza mchezo wenyewe wa soka kwa manufaa ya taifa letu, kwa maana ya kuja kuwa na timu ya taifa imara kwa siku za usoni.

Cha kufanyika ni kusajili kwa umakini mkubwa na kuhakikisha timu hazibadiliki badiliki kila inapofika mwisho wa msimu, mashabiki kuacha wachezaji huru waonyeshe uwezo wao uwanjani, muda mzuri wa maandalizi ikiwemo suala la kupatikana kwa mdhamini wa mashindano mapema na ziweke sera zitakazotoa nafasi kwa wachezaji chipukizi kuonekana.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Mifumo ya soka…….

Nilialikwa kwenye BQ nikaishia kuwa mpikaji na mchoma mishikaki..