in

Simba,Yanga mwenye kisu kikali atakula nyama 

Yanga Vs Simba

Ni Desemba 11 mwaka 2021. Ni mechi ya watani wa jadi itakayochezwa saa 11 jioni kwa  saa za Tanzania na Afrika mashariki ndani ya dimba la Benjamin Mkapa. Ni mechi ya  wakongwe wa soka na Ligi Kuu Tanzania Bara. Ni mfululizo wa Ligi kuu Tanzania Bara kwa msimu 2021/2022, ambapo timu zote mbili zinafukuzana, Yanga wapo kileleni  mwa Ligi wakiwa na pointi 19, huku Simba wakiwa nafasi ya pili kwa kujikusanyia pointi  17. 

Ni mchezo muhimu kwa pande zote mbili, kutafuta alama tatu na kutengeneza heshima.  Ili uchukue ubingwa unapaswa kuhakikisha hufungwi na timu kubwa, angalau  unatafuta alama moja.  

Unapomfunga mshindani wako unamdhibiti katika kasi yake, na hivyo mechi  zinazofuata huwa ni kuhakikisha unawabutua timu ndogo zote kadii unavyojisikia. Yanga waliwafunga Simba kwa bao 1-0 katika mchezo wa Ngao ya Jamii lililofungwa na  Fiston Mayele, lakini Simba wanaonekana kutaka kulipa kisasi. 

TANZANIASPORTS inaangazia masuala muhimu ambayo kwa kawaida mchezo  mkubwa unaohusisha timu kubwa lazima kuwe na mambo ya aina yake. ni mambo  ambayo yanaonesha uwezo,ubora,weledi,uchu na matamanio ya kunyakua ubingwa kwa  kuwachapa washindani wao wakubwa. 

WABABE WA DAKIKA 90 

Timu zote zina wachezaji wababe ndani ya dakika 90. Simba wapo wabeb kama Pascal  Wawa, Jonas Mkude,Taddeo Lweanga,Joash Onyango,Kennedy Juma na Bernard  Morrison. Yanga wanao wababe wao kama vile Khalid Aucho,Bakari Mwamnyeto,Djuma  Shaban,Yannick Bangala. Wachezaji hawa wanasifika kwa matumizi ya nguvu kwa kiasi  kikubwa. Wana uwezo wa kukabiliana na wapinzani wao kwa mabavu bila kuchoka  ndani ya dakika 90. 

WACHEZAJI WA KUCHUNGWA 

Mchezo wa aina hiyo kwa kawaida unatawaliwa na wachezaji wenye matukio ya  kushangaza au wale ambao wanapaswa kuchungwa kwa muda wote wanaokuwepo  uwanjani. 

Wachezaji wa Yanga wanafahamu ukali wa Bernanrd Morrison wa Simba na bila shaka  walimtazama katika mechi zote mbili alizocheza hivi karibuni dhidi ya Red Arrows ya  Zambia kwenye mchezo wa kufuzu hatua ya makundi ya mashindano ya Kombe la  Shirikisho la soka Afrika. 

Kasi ya Morrison na uwezo wake wa kukaa na mpura ulikuwa mwiba kwa wachezaji wa  Red Arrows. Hata walipokuja kutulia na kujairbu kumdhibiti walikuwa  wameshachelewa. Hivyo safu ya kiungo cha Yanga watakuwa na kibarua cha  kumchunga nyota huyu.  

Simba wao watataka kuhakikisha wanavuruga mipango yote inayoandaliwa kumfikia  Fiston Mayele. Kiuchezaji Mayele anategemea mpangilio wa mashambulizi na  kusogezewa mpira hadi eneo la hatari.  

Kazi hiyo inategemewa kufanywa na Feisal Salum kuwavuruga mabeki wa Simba. Ili  Feisal Salum afanye kazi yake vizuri atategemea uwezo wa Tonombe Mukoko,Zawadi  Mauya, Khalid Aucho na Yannick Bangala, na mabeki wa pembeni Kibwana Shomari na  Djuma Shaban. Kazi nyingine ya Simba itakuwa kuwadhibiti mawinga wa Yanga, Jesus  Moloko na Farid Mussa kwa sababu walikuwa mwiba katika mchezo uliopita. 

Simba nao wanaye kiungo wao Hassan Dilunga ambaye ameibuka kuwa mchezaji  hatari,kasi na mbinu nzuri za kutafuta mabao. Mabeki wa Yanga wa pembeni Djuma  Shaban,Kibwana SHomari,Mustafa Yassin na Bryson Rafael watakuwa na kibarua  kuhakikisha kiungo huyo haleti madhara.  

Dilunga amekuwa mchezaji anayebadilika kila siku, na ubora wake umeongezeka.  Katika michezo miwili ya Kombe la Shirikisho amekuwa katika kiwango kizuri  kutengeneza na kufunga. Spidi na uwezo wa kukaa na mpira pamoja na kuwasoma  wapinzani wake ni silaha ya Pablo Franco Martin. 

ROHO ZA PAKA 

Timu zote mbili zina wachezaji wenye roho ya Paka katika safu za ulinzi. Simba wanao walinzi wawili weenye roho za paka, Pascal Wawa na Joash Onyango, wakati Yanga  wanaye Bakari Mwamnyeto, Yannick Bangala na Dickson Job. Mabeki hawa Job N  Mwamnyeto wamekuwa wagumu kupitika na wameonesha umahiri katika mechi  mbalimbali za Ligi Kuu. Mtihani walionao washambuliaji wa Simba na Yanga ni  kuwazidi maarifa mabeki hao kisha kupachika mabao. Je itawezekana? 

WAKALI WA NDANI YA BOKSI 

Fiston Mayele sio mshambuliaji wa kukokota mpira kutoka mbali kama ilivyo kwa  Herieter Makambo. Mayele kwa Yanga na Medie Kagere kwa Simba wanapenda  kujipanga katika boksi, kisha kupata nafasi ya kutupia mabao. Kagere na Mayele sio  aina ya washambuliaji ambao wanakokota mpira kutoka mbali kuingia eneo la hatari,  badala yake hawa wanatupia wavuni wakiwa ndani ya boksi. Kuwaacha katika eneo hilo  bila kuwazuia ni hatari kwa timu pinzani. 

USHINDANI MKALI

Simba hawataki kufungwa tena na Yanga kama ilivyokuwa kwenye mchezo wa Ngao ya  Jamii Septemba 29 mwaka huu. Yanga hawataki kufungwa na wanataka kuendeleza  ubabe kwa kuwachapa watani hao. Simba watataka kurudia kile walichokifanya Julai 7  kwenye fainali ya Kombe la ASFC kwenye uwanja wa Lake Tanganyika kwa kuwachapa  bao 1-0 lililofungwa na Luis Miquissone. Yanga nao watataka kuendeleza ubabe kama  ule waliofanya kwenye mashindano ya Kombe la Mapinduzi visiwani Zanzibar ambako  waliifunga Simba kwa penati 4-3. Simba watakuwa na uchungu mwingine wa Julai 3  mwaka huu baada ya kukubali kipigo cha bao 1-0 toka Yanga lililofungwa na kiungo  mkabaji Zawadi Mauya. 

MIFUMO YA KUAMUA MATOKEO 

Makocha wa timu zote mbili watakuwa na kibarua cha kuchagua mifumo sahihi ya  kuwafunga wapinzani wao. Timu zote mbili zimekuwa katika mifumo mitatu rasmi; 3-4- 3, 4-3-3 na 4-2-3-1. 

Mifumo yote hiyo inatengeneza mshambuliaji wa kucheka na nyavu akiwa peke yake  huku akizungukwa na mawinga na viungo wa kupachika mabao. 

Pablo Franco Martin na Nasredine Nabi watakuwa na kibarua kigumu kuwatuliza  wachezaji wao kwa sababu mechi kubwa kama hiyo huambatana na matukio ya  kushangaza,presha na kusababisha kupoteza umakini ndani ya dakika 90. Vyovyote vile  itakavyokuwa ni mechi kubwa na yenye kila aina ya shinikizo kwa makocha,viongozi na  wachezaji. 

MAREFA KUNG’ARA? 

Heri Sassi kutoka mkoa wa Dar es salaam ndiye mwamuzi aliyekabidhiwa jukumu la  kuziamua Yanga na Simba. Ni mwamuzi ambaye anakabiliwa na kibarua kigumu  kusafisha nyota ya waamuzi wa Ligi kuu Bara baada kukosolewa kutokana na maamuzi  mabovu waliyofanya mara kwa mara. Katika mchezo huo waamuzi wa pembeni yaani  washika vibendera ni Kassim Mpanga kutoka Dar es salaam na Hamdani Said kutoka  mkoani Mtwara, wakati mwamuzi wa akiba ni Ahmada Simba kutka mkoani Kagera. Bila shaka matokeo yataonekana kama wamefanikiwa kuonesha umahiri au watafeli.

Report

Written by Mark Mpangala

*Markus Mpangala ni Mhariri, Mwandishi wa Makala Maalumu, Mwanahabari,Mwanablogu,Mwanafasihi na Mwanasafu, ambapo kwa kipindi cha miaka 12 amefanya kazi katika vyombo vya habari mbalimbali vikubwa na vidogo nchini Tanzania katika Michezo, Siasa, Elimu na utalii. Pia ni mchambuzi mchangiaji wa masuala ya siasa na utawala bora katika idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC SWAHILI). Ni mhariri na mhamasishaji wa usomaji wa vitabu*

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0
Tanzania Sports

Refa ameiba matokeo ya Simba na Geita Gold FC

Divock Origi

Jurgen Klopp anambagua Origi?