in , , ,

Rais Barcelona aachia ngazi

*Shabiki apiga polisi kumtafuta Ferguson

Homa ya soka inaendelea kuzitesa nchi za Hispania na Uingereza, ambapo Rais wa Klabu ya Barcelona, Sandro Rosell ameachia ngazi huku mashabiki wa Manchester United wakiweweseka.

Rosell amejiuzulu baada ya kukumbwa na kashfa ya usajili wa mshambuliaji kinda kutoka Santos ya Brazil, Neymar, ambapo inadaiwa alidanganya juu ya bei yake.

Rais huyo alishitakiwa na mwanachama wa klabu hiyo mahakamani kwa madai kwamba bei aliyonunuliwa mchezaji huyo si ambayo ilitangazwa na kwamba rais ni mfujaji wa fedha zao.

Uamuzi huo pia unakuja wakati Mahakama ya Hispania ikianza uchunguzi wake juu ya mauzo na manunuzi ya Neymar na madai kwamba amefuja pauni milioni 48.6.

Hata hivyo, Rosell anasema kwamba kila kitu kilifanyika kwa usahihi na yupo tayari kutoa ushahidi na ufafanuzi mbele ya jaji.
Uongozi wa juu wa Barca sasa unashikwa na Makamu wa Rais, Josep Maria Bartomeu na haijulikani kama mabadiliko hayo yatawaathiri Barca wanaoongoza ligi lakini wakiwa wamekabwa koo na Atletico Madrid na Real Madrid.

SHABIKI AITA POLISI KUMTAFUTA FERGUSON

IMG_2476

Msimu mbaya wa Manchester United umeshuhudia shabiki wa klabu hiyo akipiga simu polisi (999) akimtafuta kocha aliyeachia ngazi mwaka jana, Sir Alex Ferguson.

Shabiki huyo ambaye alikuwa amelewa lakini alifikisha ujumbe unaoaminiwa kuwa wa wengi, alitaka Fergie arudi Old Trafford kuchukua nafasi ya Mskochi aliyemwachia kiti, David Moyes ambaye maji yanaelekea kumfika shingoni.

Shabiki huyo alipiga simu Kituo cha Polisi cha Greater Manchester usiku wa saa 4.30 Jumatano akilalamikia matokeo ya Mashetani Wekundu kufungwa na Sunderland na kutolewa kwenye Kombe la Ligi.

Polisi wa Manchester wamesema ni kweli kwamba inatia uchungu na kuleta msongo wa mawazo timu unayoipenda inapofungwa lakini wakakumbusha kwamba namba ‘999’ inatakiwa kupigwa kwa ajili ya masuala ya dharura tu.

Hapakuwa na dharura yoyote kwa United kufungwa, kwa sababu ilishafungwa zaidi ya mechi nne hapo Old Trafford na mwelekeo wao ulikuwa si mzuri, lakini hata kama ingekuwa ghafla polisi hawahusiki.

Man U walifungwa 2-1 kwa penati na hao Black Cats baada ya matokeo ya mechi zao mbili kwenda 3-3 na penati nyingi kukoswa na wachezaji wanaochukuliwa kuwa mahiri kwenye mchezo huo mkali.

Jamaa aliyepiga simu polisi aliulizwa iwapo alitaka kuripoti tukio la jinai naye akasema ndiyo, ila akaongeza kwamba alitaka kuzungumza na Fergie.

“Ndio. Nataka kuripoti tukio la jinai, na jinai yenyewe ni kwamba Manchester United wamepigwa, walikuwa hovyo kabisa, matokeo haya siyo, walipewa muda wa ziada na kwa kweli huu ni upuuzi na uchafu mtupu, je, Polisi mnaweza kutusaidia kumrudisha Ferguson?”

Polisi walimwambia shabiki huyo kwamba kama anamtaka Ferguson ajaribu kupiga simu klabuni Manchester United ambako huenda angeweza kumpata lakini pia polisi ikahadharisha kwamba hawana uhakika kama angempata. Shabiki huyo ameonywa lakini hatashitakiwa.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Yanga ” Waturuki” warudi kileleni VPL