in , , ,

PIERRE AMEKUJA SIMBA MUDA AMBAO SIYO SAHIHI

PIERRE AMEKUJA SIMBA MUDA AMBAO SIYO SAHIHI

Rasmi Simba jana imeingia mkataba na kocha Mfaransa Pierre Lenchantre
na anatarajiwa kuanza kazi na kikosi cha Simba jumanne.

Ni kocha mwenye elimu kubwa ya ukocha , hapana shaka ana mafanikio
makubwa pia katika mpira wa Afrika.

Mshindi wa Afcon mwaka 2000 akiwa na Cameroon na akafanikiwa kuwa
kocha bora wa CAF mwaka 2001.

Elimu yake kubwa ya UEFA pro licence aliionesha kwa vitendo uwanjani
akiwa anaifundisha Cameroon.

Sifa kubwa zikawa juu yake na heshima kubwa akawa nayo.

Ni moja ya makocha wenye mafanikio na soka la Afrika.

Siyo mgeni na mpira wa Afrika kwani ashafanikiwa kufundisha mpira
Cameroon, Congo Brazzavile , Tunisia.

Hana ugeni wowote na mpira wetu wa Afrika, ni moja ya faida kubwa
ambayo Simba wanaenda kunufaika nayo kutoka kwa huyu ƙkocha.

Simba imekuwa timu yenye bahati kubwa ya kupata makocha wenye historia
nzuri na mpira wa Afrika.

Hata kocha mkuu aliyepita, Joseph Omog alikuwa na historia nzuri na
soka la Afrika.

Aliwahi kushinda kombe la shirikisho barani Afrika akiwa na AC
Leopards ya Congo.

Akafanikiwa kuwa kwenye orodha ya makocha watatu ambao waliingia hatua
ya mwisho ya kuwania tunzo ya kocha bora wa Afrika mwaka 2012.

Lakini alipofika Simba hakufanikiwa kwa kiasi kikubwa kama ambavyo
alikuwa AC Leopards.

Inawezekana mashabiki wa Simba kwa sasa wanamatumaini makubwa na kocha
Pierre Lechantre.

Wakiamini kuwa anaweza kuwa tiba sahihi kwao wao kwenye ugonjwa wa
kutobeba ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania kutokana na historia yake
inavyombeba.

Inawezekana ikawa sahihi kwao kuwa na matumaini kwao, lakini inaweza
ikawa kamari pia.

Wanatakiwa waelewe hivyo kwamba hii ni kamari ambayo inaweza ikawa
kweli au isiwe kweli.

Na kamari hii inaonekana kuwa ngumu kufanikiwa kuwa kweli kwa sababu
ya kipindi ambacho kocha huyu kaja.

Kaja kipindi ambacho timu ipo katikati ya Ligi. Lazima anapokuja
kwenye kikosi hiki atajaribu kuingiza falsafa mpya za kwake
anazoziamini ili timu ifanye vizuri.

Falsafa hii inaweza ikawa tofaufi na watangulizi wake ( Joseph Omog na
Masoud Djuma)

Hivo wachezaji watalazimika kuanza kujifunza kitu kipya tofauti na cha awali.

Kwa maana nyingine timu inaanza upya tena.

Tuliona hiki kitu kipindi ambacho Joseph Omog anaondoka, Kocha Masoud
Djuma ilimchukua takribani mechi tano kuhakikisha falsafa yake angalau
inaanza kueleweka na wachezaji wa Simba.

Kocha huyu mpya anakuja na kitu chake kipya, kitu ambacho kitachukua
muda kueleweka kwa wachezaji.

Haijalishi muda ambao utatumika wachezaji kuelewa, uwe muda mfupi au
mrefu, muda ambao Simba itakuwa inasubiri falsafa za kocha huyu ziweze
kueleweka vizuri kwenye kikosi cha Simba ndiyo muda ambao wapinzani
wake watautumia kumzidi.

Tukunbuke mpaka sasa Simba yuko mbele ya alama mbili mpaka sasa dhidi
ya Azam FC, ni alama chache ambazo hazimpi nafasi ya yeye kujiona yuko
huru kukimbia katika mwendo anaoutaka yeye.

Nilikuwa nafikiria kama Simba wangeamua kumwachia kocha Masoud Djuma
amalize ligi ya msimu huu ungekuwa uamuzi wa busara sana kwa sababu
mpaka sasa hivi inaonesha kuna kitu kikubwa amekiweka ndani ya kikosi
cha Simba.

Kuna maelewano ameyajenga kati yake na wachezaji.

Wachezaji wanacheza kwa kuelewana ndani ya uwanja.

Wachezaji wanayofuraha kwa sasa ndani ya mfumo wa kocha Masoud Djuma.

Wanakuja tena kuhamishwa na kwenda katika mfumo mpya wa kocha mpya,
hatujui kama watakuwa na furaha au La kucheza ndani ya mfumo mpya wa
kocha Pierre Lenchantre.

Na hii pia inachangia kuwachanganya wachezaji kwa sababu ndani ya
msimu mmoja mchezaji anakuwa chini ya makocha watatu wenye falsafa
tofauti.

Mchezaji anakuwa mtu wa kuanza upya kila mara.

Hivo kuepukana na vyote hivi naamini kocha Masoud Djuma alikuwa mtu
sahihi kuachiwa timu mpaka mwishoni mwa msimu mwa msimu huu, ujio wa
Pierre Lenchantre katikati ya ligi haukuwa wakati mzuri kwa timu ya
Simba.

Ingekuwa wakati mzuri kwa Pierre Lenchantre kuanza kazi msimu ujao ili
kuwa na muda mzuri wa yeye kufundisha falsafa anazoziamini.

Muda huu Simba inapresha ya kupata ubingwa wa Ligi kuu, hivo ni ngumu
kwa Pierre Lenchantre kuweka falsafa zake huku akiwa na presha kubwa
ya ubingwa

Report

Written by Martin

Martin Kiyumbi ni mchambuzi wa habari za michezo na mbunifu wa maudhui.

Martin Kiyumbi amewahi kufanya kazi za uchambuzi kwenye vituo mbalimbali vya habari kama Tanzaniasports (tovuti ya habari za michezo ), Jembe FM , Radio Free Africa na TVE.
Martin Kiyumbi anapatikana kwenye e-mail ya [email protected]

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

YANGA FANYENI HIVI KWANZA…..

Tanzania Sports

MICHAEL CARRICK KWENYE UBETI MMOJA NA FUNDI AKILI