in , , ,

NILICHOKIONA KWENYE MECHI ZA LIGI YA MABINGWA BARANI ULAYA ( UEFA)


*Mfumo wa kutumia mabeki watatu uliwagharimu kwa kiasi kikubwa
Manchester City mwanzoni mwa mechi hii*

Kumpanga John Stones, Otamendi na Sagna kama mabeki wa kati ilikuwa
haina faida kwao kwa sababu, moja John Stones bado hajakomaa anatakiwa
kucheza chini ya uangalizi ili apunguze makosa yake binafsi, na njia
nzuri ya kumfanya acheze chini ya uangalizi ni Kumchezesha kwenye
mfumo wa mabeki wanne ili apate uangalizi kutoka kwa beki mwingine wa
kati. Pili, mfumo huu haukuwa na faida kwa upande wa pembeni kwa
sababu hakukuwepo na mabeki ambao wangesaidia kupandisha mashambulizi
ya Timu. Ingizo la Zableta lilileta uhai mkubwa sana kwenye safu ya
ulinzi ya Manchester City.

Kuna unafuu kwenye eneo la golikipa, ila ugonjwa bado haujapona.
Pamoja na kwamba Caballero aliokoa Penalti lakini hakuonesha ubora wa
kuibeba timu, pia alikuwa na makosa mengi binafsi ambayo kwa kiasi
kikubwa yalisababisha goli la Mbappe.

Kama ilivyo kwenye ugonjwa wa eneo la Golikipa la Manchester City,
pia eneo la beki la Manchester City lilikuwa na tatizo pia, John
Stones na Otamendi wamelikuwa siyo imara na hii ni kwa sababu mbili,
moja Otamendi siyo kiongozi sahihi wa kumuongoza John Stones, pili
John Stones bado hajawa mkomavu ndiyo maana anakuwa na makosa mengi
binafsi.

Uwepo wa Sane na Sterling kule mbele umeongeza pumzi ya uhai wa eneo
la ushambuliaji wa Manchester City, kwa sababu wote wawili walikuwa
na kasi pia walikuwa wazuri sana kwenye kutengeneza nafasi za magoli
pamoja na kufunga magoli kitu ambacho kilileta mgawanyo mzuri wa
magoli ukijumlisha na ya Kun Aguero.

Ukimzungumzia Kun Augero katika mechi ile utakiona kitu kimoja ,
uzoefu wake ulikuwa msaada sana kwa Manchester city.

Kwenye kumbukumbu zako unaweza ukawa unawakumbuka kina Kondogbia,
Martial, Carrasco. Hiki kilikuwa kizazi kilichokuwa kimetengenezwa
lakini kikauzwa kabla hakijawapa kombe lolote Monaco. Ila muda huu
kuna kizazi kingine ambacho kuna uwezekano kikawapa Monaco kombe
pamoja na pesa kwa pamoja.

Bakayoyo, Fabinho, Bernaldo Silva, Mbappe na vijana wengi wa Monaco
ambapo kwa kiasi kikubwa wana umri mkubwa ndiyo walikuwa na msaada
mkubwa kwenye hii mechi.

Kasi ya Mbappe na Bernaldo Silva ilikuwa na madhara makubwa sana kwa
upande wa pembeni kitu ambacho kilisababisha kuwapa presha mabeki wa
Manchester City.

Kitu pekee ambacho kiliwagharimu Monaco kwa kiasi kikubwa ni kwamba,
walishindwa kuhimili presha ya mashambulizi ya Manchester City.

Mwanzoni walifanikiwa kuwabana Sane na Sterling wasitembee kwa kiasi
kikubwa lakini kadri muda ulivyokuwa unaenda umakini ulikuwa unapungua
kwenye jukumu hili.

Mfano kuna goli ambalo walifungwa kutokana na wao kwenda wote
kushambulia na kisha wakafanyiwa shambulizi la kushtukiza
lililosababisha goli kwao.

Pia mabeki wao mwishoni walikuwa na Marking mbovu iliyosababishwa na
wao kutojipanga vyema wakati wanashambuliwa na Manchester City.

BAYER LEVERKUSEN vs ATLETICO MADRID.

Atletico Madrid wanapata ushindi wao wa kwanza wakiwa Ujerumani baada
ya kushindwa kuupata kwenye safari zao tatu walizoenda Ujerumani.
Vitu pekee ambavyo viliwasaidia kwa kiasi kikubwa Atletico Madrid ni
viwili, cha kwanza ni mbinu za Diego Simione katika kipindi cha
kwanza.Pamoja na kwamba Bayer Leverkusen hawakuwatia presha Atletico
Madrid kwa kiasi kikubwa kwa kipindi cha kwanza lakini walifungwa kwa
mashambulizi ya kushtukiza ambapo wao hawakuwa wazuri kwenye kuzuia
mashambulizi ya kushtukiza.

Kitu cha pili kilichomaliza mechi hii ni kasi ya Carrasco, Antoinne
Griezman, Gameiro pamoja na Saul kucheza eneo ambalo huru ambalo kwa
kiasi kikubwa lilimsaidia kuwa huru zaidi ingawa hakuwa na kasi kubwa
kulinganisha na hao wenzake watatu.

Kwa muda mrefu Atletico Madrid walikuwa wakimtafuta mshambuliaji
ambaye atacheza pamoja na Antoinne Griezman kwa Ushirikiano mkubwa.
Gameiro amekuwa mtu sahihi kwa hili, Ushirikiano wao kwa siku za hivi
karibuni utatengeneza safu hatari ya ushambuliaji.

Inawezekena Chicharto ndiye mshambuliaji ambaye alikuwa akiangaliwa
kama msaada mkubwa sana kwenye mechi ile kwa ajili ya kuwakomboa Bayer
Leverkusen, lakini mabeki wa Atletico Madrid kwa kiasi kikubwa
walimkaba Man to Man. Tukumbuke siyo mshambuliaji ambaye ana uwezo wa
kupambana na mabeki zaidi ya kuvizia.Walichokifanya Atletico Madrid ni
kuziba mianya ambayo ingempa nafasi yeye kuvizia

SEVILLA VS LEICESTER CITY.

Leicester City

Kuna vitu ambavyo vilikuwa vinawafanya Leicester City wawe katika hali
ngumu sana hasa hasa kipindi cha kwanza.

Ndindi ni mzuri sana kwa kukaba, kitu pekeee ambacho anakosa ni
kuanzisha mashambulizi. kitu ambacho kilikuwa kinamsababisha
DrinkingWater awe anarudi kuchukua mpira ili aanzishe mashambulizi
badala ya kupokea mipira kutoka kwa Ndindi kitu ambacho kilikuwa
kinasababisha watu wa mbele kutokuwa na uwezo wa kupata mipira kwa
wingi na kuifanya Sevilla iwe ina miliki mpira kwa asilimia kubwa.

Pamoja na kwamba Leicester City inamkosa mtu mwenye kariba ya Kante,
lakini Leicester bora yenye safu imara ya ushambuliaji inamwihitaji
Mahrez aliye kwenye kiwango kikubwa. Lakini kwa mechi ya jana Mahrez
alikuwa amekabwa na mabeki wa Sevilla kitu ambacho kilichosabisha safu
ya ushambuliaji ya Leicester City kutokuwa hai.

Musa alikuwa na workrate kubwa tatizo lake kubwa ni kwenye maamuzi ya
mwisho, yani kwenye kufunga pamoja na kutoa pasi za mwisho. Kwa hali
hii Leicester City walimkosa kwa kiasi kikubwa Slimani kwenye mechi ya
jana.
Sevilla walikuwa na nafasi kubwa sana hasa hasa kipindi cha kwanza
kupata magoli mengi lakini hawakutumia nafasi ile vizuri.

Ushirikiano wa Nz’onzi na Samir Nasri ulikuwa mkubwa sana hasa hasa
kipindi cha kwanza, hali iliyowapa ugumu kwa kiasi kikubwa Ndindi
pamoja na Drinking Water.

Kasper Schmeichel ndiye aliyekuwa mhimili mkubwa kwa upande wa
Leicester City katika mechi ya jana. Utulivu wake ulimfanya afanye
saves ambazo ziliisaidia timu kwa kiasi kikubwa.

FC PORTO VS JUVENTUS.

Juventus

Kitu pekee ambacho kilikuwa kinamuumiza kichwa Massimiliano Allegri
katika mechi hii ni jinsi gani ya kuziba pengo la Leornado Bonucci.
Alichokifanya ni kubadili mfumo na kutumia mfumo wa 4-2-3-1 ambao
ulimpa nafasi ya kutumia mabeki wanne badala ya watatu. Kitu ambacho
kilifanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Pjanic alibadikika sana kwenye mfumo huu wa 4-2-3-1 , tumekuwa
tukimfahamu tangia akiwa Roma kuwa ni mchezaji ambaye ni mzuri akiwa
katika eneo la kiungo wa kushambulia, lakini Allegri alimbadilishia
majukumu na kwa kiasi kikubwa aliyatimiza, uwezo wake mkubwa wa kukaba
na kutoa pasi za uhakika ndiyo ulikuwa msaada mkubwa sana kwa Juventus

Kadi nyekundu ya Alex Telle iliwatoa kwenye Upiganaji Fc Porto kwa
asilimia kubwa kwa sababu, awali walikuwa na uwezo mkubwa sana wa
kufanya mashambulizi.

Lakini baada ya kadi nyekundu walirudi nyuma na kujilinda kwa muda
mwingi wa mchezo.

Kwenye Mechi mpira unapojilinda kwa muda mwingi umakini hupungua kadri
muda wa mchezo unavyozidi kwenda. Na umakini ukipungua husababisha
safu ya ulinzi na wachezaji wengi kufanya makosa binafs.

Na ndicho kitu kilichotokea.

Fc Porto walifanikiwa kujilinda vyema kwa muda mrefu, lakini umakini
ulipungua na kusababisha wafungwe.

Report

Written by Martin

Martin Kiyumbi ni mchambuzi wa habari za michezo na mbunifu wa maudhui.

Martin Kiyumbi amewahi kufanya kazi za uchambuzi kwenye vituo mbalimbali vya habari kama Tanzaniasports (tovuti ya habari za michezo ), Jembe FM , Radio Free Africa na TVE.
Martin Kiyumbi anapatikana kwenye e-mail ya [email protected]

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote
Tanzania Sports

Jinamizi kwa kipa aliyekula uwanjani

Tanzania Sports

Rooney kuhamia China?