in , , ,

NI ELIMU GANI TUNAIPATA KUTOKA KWA ICELAND?

Iceland inakuwa nchi ndogo zaidi kupata nafasi ya kushiriki kombe la
dunia mwaka 2018 nchini Russia.

Siyo mara ya kwanza kwao kama nchi ndogo kushiriki katika mashindano
makubwa ngazi ya timu ya taifa. Mwaka 2016 pia walikuwa nchi ndogo
zaidi kushiriki kombe kubwa kwa kushiriki Euro 2016 nchini Ufaransa.

Waliishia hatua ya robo fainali ambapo walitolewa na wenyeji ambao
walifika fainali.

Iceland katika michuano hii ya Euro 2016 ilifanikiwa kwa kucheza na
wanafainali wa michuano hiyo, ikianza na Ureno ambayo walikutana nayo
katika hatua ya makundi.

Ambapo walimaliza hatua ya makundi bila kufungwa hata mechi moja, na
mwisho wa siku ikae nda kuwatoa England katika michuano hii ya Euro.

Yalikuwa mafanikio makubwa sana kwa timu ambayo miaka minne iliyopita
ilikuwa nafasi ya 133 katika zile nafasi za msimamo wa FIFA.

Ni nchi ndogo yenye idadi ya watu 334,000 ambapo watu wengi
hawakutegemea mafanikio yao ya haraka kama kushiriki katika michuano
mikubwa (Euro na kombe la dunia) na kupanda katika nafasi 100 katika
nafasi za FIFA.

Mwanga wa mafanikio ya nchi hii ulianza kuonekana katika mwaka 2013
ambapo walienda katika play off na kufungwa kitu ambacho kilisababisha
wao wasifuzu kombe la dunia nchini Brazil katika hatua za mwisho.

Njia hii ya mafanikio ya mpira ya Iceland ilianza kutengenezwa
mwanzoni wa mwaka 2000, ambapo miaka 15 baadaye matunda yameanza
kuongezeka.

Serikali ya nchi ya Iceland ilianza kutengeneza sera nzuri ya michezo
ambayo ilisaidia mtoto mwenye umri kuanzia miaka 4 anaanza kufundishwa
michezo.

Sera hii iliwezesha kuzalisha wachezaji wengi sana nchini Iceland
mpaka ikafika wakati Iceland ikawa na wachezaji 22,000 ambao walikuwa
wamesajiliwa kama wachezaji wa kulipwa nchini Iceland, ingawa kulikuwa
na wachezaji wengine zaidi ya 10,000 ambao walikuwa wanacheza mpira
bila kusajiliwa.

Idadi hii ilikuwa inatoa maana halisi ya kuwa Iceland ilikuwa na
wachezaji zaidi ya elfu thelathini (30,000) kati ya watu 334,000 ambao
ilikuwa idadi ya watu nchini Iceland.

Wachezaji hawa walikuzwa katika misingi ya kisomi , kwa sababu
walifundishwa mpira katika shuleni kulingana na sera ya Iceland, hivyo
walikuwa katika misingi ya kuwa na mafanikio zaidi katika misingi
sahihi.

Iceland ina makocha zaidi ya 8000 ambao wana leseni ya UEFA daraja A
na leseni ya UEFA daraja B ambao wamekuwa wakihusika kufundisha watoto
pamoja na timu za Iceland.

Mwaka 2009 idadi kubwa ya vijana kutoka nchini Iceland walienda nchini
Uingereza kwenda kusomea leseni ya ukocha.

Idadi kubwa ya makocha nchini Iceland ni vijana, tukumbuke kundi la
vijana linaendana sambamba na mahitaji ya soka la kisasa ambalo
limeegemea zaidi kwenye mifumo na mbinu za kisasa. Kitu ambacho
kimewasaidia kuzalisha wachezaji ambao wanaendana na mbinu pamoja na
mifumo ya kisasa.

Iceland ilifanikiwa kuzalisha makocha wengi, kati ya nchi ambayo kocha
anahudumia wachezaji wachache ni Iceland (per capita)

Kuwa na idadi kubwa ya makocha haiwezi kuwa sababu tosha kwa nchi
kuendelea katika soka, ingawa ni moja ya sababu ya msingi katika
maendeleo ya soka lakini siyo sababu tosha ya maendeleo ya soka.

Serikali ya Iceland iliandaa mazingira mazuri kwa ajili ya wachezaji
wa Iceland kucheza mpira kwa kujenga viwanja.

Siyo serikali peke yake ambayo ilihusika katika ujenzi wa viwanja, ila
ilishirikiana na timu za Iceland pamoja na wadhamini mbalimbali
kuhakikisha kuna idadi kubwa ya viwanja.

Iceland ilifanikiwa kujenga viwanja 23 vikubwa , viwanja 7 vya ndani
na viwanja 200 vidogo ambavyo vilikuwa na nyasi bandia.

Walijenga viwanja vya ndani kwa sababu ya baridi Iliyopo nchini
Iceland, ambapo kuliwawezesha wachezaji kufanya mazoezi katika viwanja
hivi vya ndani katika hali nzuri tena bila matabaka yoyote yale.

Report

Written by Martin

Martin Kiyumbi ni mchambuzi wa habari za michezo na mbunifu wa maudhui.

Martin Kiyumbi amewahi kufanya kazi za uchambuzi kwenye vituo mbalimbali vya habari kama Tanzaniasports (tovuti ya habari za michezo ), Jembe FM , Radio Free Africa na TVE.
Martin Kiyumbi anapatikana kwenye e-mail ya [email protected]

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote
Tanzania Sports

VITU MUHIMU KWENYE MECHI ZA KUFUZU KOMBE LA DUNIA NCHINI RUSSIA 2018

Tanzania Sports

Arsenal: Kichapo stahiki kwa Arsรจne Wenger