in

LoveLove SurprisedSurprised

Moro aigharimu Yanga VPL

Moro kaigharimu Yanga

Mchezo wa jihadi wameuonesha timu ya Yanga baada ya kulazimisha sare ya kufungana goli 1-1 katika uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma dhidi ya JKT Tanzania.

Huenda ukashangaa kuona Moro kaigharimu Yanga ukawa na shauku ya kujua nini amefanya wakati mchezo umeisha kwa sare.

Yanga inaelekea katika mchezo mgumu dhidi ya mpinzani wake katika kugombania nafasi ya pili ligi kuu Tanzania Bara ambaye ni Azam FC.

Moro amefanya tukio la ajabu ambalo sio rahisi kumuelewa kwanini amefanya hivyo hasa kwa kuwa yeye ni ‘Professional’ amempiga teke la mgongo Mwinyi Kazimoto na kukosa mchezo dhidi ya Azam FC na michezo mingine mtawaliwa.

Kukosa mchezo dhidi Azam FC ni pigo kubwa sana kwa Yanga ambayo imewekeza nguvu zake katika kupigania angalau nafasi ya pili huku timu hiyo ikimuamini sana Moro kwa uchezaji wake na jitihada binafsi.

Ni kweli Moro amekuwa mchezaji muhimu ndani ya kikosi cha Yanga msimu huu amecheza vizuri na kukosekana kwake kunaweza kuigharimu timu hiyo katika mechi ambazo yeye hatokuwepo.

Moro-Redcard

Hapa nafikiria kwanini amefanya vile, natamani kukaa katika ubongo wake kwanini alicheza kunfuuu katika soka? Hivi hakujua kuwa angemvunja kiuno mwenzake ?

Hayo maswali yananinyima raha sana sijui kama ataweza kusahaulika kwa tukio bovu kama lile. 

Haya sasa ametolewa kwa kadi nyekundu atakosa mchezo wa Azam haoni kama ni pengo kubwa, unaweza kusema Yondani na Makapu wapo ila ule ubora wa Moro haujauona hili pia unajiuliza?

Moro ukifungiwa na baadae kufunguliwa lazima umuombe radhi Mwinyi Kazimoto na soka la Tanzania umekosea sana.

Hapa najiuliza tena hivi Yanga wanautaratibu wa kuwachukulia hatua wanaopata kadi nyekundu kama aina hii? Huenda  makala yangu ikawa na maswali mengi kuliko majibu, hii yote kukosa weledi kwa wanaojiita ‘maproo’.

Hapa wenye timu wanaweza kuhoji tukio la Pascal Wawa na Ditram Nchimbi kwanini sikulielezea, hayo yule pia alipuyanga sana na niliwahi kumsema kwa aina nyingine maana hao ndio wachezaji wetu wanaosajiliwa kutoka nje.

Hebu tuangalie tukio lilivyotokea mchezaji wa Yanga alikatwa na kuanguka chini aliyemkata mchezaji wa JKT Tanzania alimfanyia uhuni kwa kumkinda nyota wa Yanga licha ya kuanguka tayari bado aliendelea kumsakama pale chini.

Ndipo akatokea Yondani kuamua kesi wakati hayo yakiendelea Kazimoto naye akatokea na kuamua kesi ndio hapo Moro akatokea alipotokea na kuruka ‘Kung fuu’ Karate katika kiuno cha Kazimoto.

Kazimoto alionekana kukasirika kutaka kumtwanga ngumi Moro nahisi pia alitoa lugha chafu ndio maana naye akapata kadi nyekundu.

Kama bodi ya ligi ikimfungia Moro huenda akakosa mchezo wa kombe la FA dhidi ya Kagera Sugar baada ya kucheza na Namungo, hivi akikosa mchezo huo wa kombe ambalo linaweza kuwapeleka kucheza kimataifa hajaigharimu Yanga ?

Baada ya yote turejee katika mchezo wenyewe, JKT Tanzania walikuwa wazuri zaidi ya Yanga hasa katika utimamu wa mwili pamoja kumiliki mpira.

Waliweza kucheza kwa kujiamini sielewi kama ‘lockdown’ iliwapata hawa JKT Tanzania, walikuwa na mazoezi sana kila mchezaji alioneka kuwa katika kiwango bora kabisa na hii ndio maana halisi ya timu.

Walichokifanya walipitia upande wa kushoto ambao alicheza Adeyun Saleh, huenda waligundua udhaifu wa Yanga upande huo.

Goli lao alilofunga Michael Aidan limejaa ufundi wa hali ya juu kwani shuti la umbali wa yadi 45 nakuingia moja kwa moja katika goli la Yanga likimshinda goli kipa Metacha Mnata.

JTK Tanzania walijiandaa kiakili na walijua kabisa watakutana na Yanga ambayo imesheheni nyota wazuri wanaohitaji matokeo ili wawashawishi mabosi wao kuwapa mkataba mwingine, lengo lao limetimia.

Michael Aidan atakumbukwa sana katika akili ya Mnata huko katika maisha yake huenda akawa na lakusema siku akiulizwa goli gani alilofungwa analikumbuka katika historia yake ya soka.

Yanga waliingia uwanjani wakiwa na kumbukumbu nzuri ya ushindi katika raundi ya kwanza wa magoli 3-2 ila walijua kuwa mchezo utakuwa mgumu kwa upande wao.

Walicheza kwa kadiri walivyoweza ila bado wanahitaji muda zaidi ili wacheze kama timu moja.

Yanga wanakosa watu washoka pale mbele wakuweza kuwapa furaha Wanayanga, safu ya mbele iliyo ongozwa na Ditram Nchimbi haikufanya maajabu kabisa.

Niliwasikia watu wa kibanda umiza wakisema kuwa zile ‘Sub’ alizofanya Luc Aymael hazikuwa nzuri Mrisho Ngasa alitakiwa apate nafasi zaidi kuliko Yikpe.

Timu hiyo imefikisha alama 55 bado ipo nafasi ya tatu ikisiburi mchezo wao dhidi ya Azam FC siku ya jumapili.

Wakati huo huo itaenda kucheza na Namungo FC katika ligi kuu Bara nawaza sana michezo hii miwili ya Yanga.

Kwa namna hii sasa Simba ubingwa ni swala la muda tu na wamelipa kuchukua mara tatu mfululizo kama walivyofanya Yanga misimu mitatu nyuma.

Report

Written by Amini Nyaungo

For the past 9 years, I have been working as the Sports news Journalist in online and print media this experience help me to be utilized by the different sports events where I have got chances to the media as the football pundit in different media in Tanzania.

What do you think?

75 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0
Liverpool FC

Faida mechi za nyumbani

Mwamuzi wa mpira wa wavu

Yupo wapi refa bora wa dunia apewe tuzo yake?