in , , ,

Marufuku kuingia mpirani kwa Dezo! TFF


*TFF YAONDOA ‘FREE PASS’ MPIRANI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeondoa utaratibu wa wadau wake kuingia bure kwenye mechi kwa kutumia tiketi maalum (free pass).

Kutokana na uamuzi huo hakutakuwa tena na pasi za bure kwa ajili ya kushuhudia mechi zilizo chini ya usimamizi wa moja kwa moja wa TFF katika viwanja mbalimbali nchini.

Uamuzi huo umetokana na ukweli kuwa free pass zimekuwa zikipunguza au kuchukua mgawo wote wa TFF kwenye mechi, na wakati mwingine Shirikisho hulazimika kutoa fedha za ziada kugharamia pasi hizo.

Pasi zote ambazo imekuwa ikitoa kwa wadau wake hukatwa katika mgawo wa TFF katika mechi husika. Shirikisho hivi sasa linapata asilimia nne tu ya mapato katika mechi za Ligi Kuu, ligi ambayo hivi sasa inaendeshwa na Kamati yake ya Ligi.

RUVU SHOOTING KUIKABILI YANGA VPL
Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Machi 16 mwaka huu) kwa mechi tatu ambapo Yanga itakuwa mgeni wa Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwamuzi Jacob Adongo kutoka Musoma mkoani Mara ndiye aliyepewa jukumu la kuchezesha mechi hiyo namba 146. Adongo atasaidiwa na Anold Bugado wa Singida na Milambo Tshikungu kutoka Mbeya wakati mwamuzi wa mezani ni Hashim Abdallah wa Dar es Salaam.

Mtathmini wa waamuzi ni Army Sentimea wakati Kamishna wa mechi hiyo inayokutanisha vinara Yanga na Ruvu Shooting inayoshika nafasi ya saba ikiwa na pointi 29 chini ya ukufunzi wa Charles Boniface Mkwasa na Msaidizi wake Selemani Mtungwe ni Emmanuel Kavenga kutoka Mbeya.

Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya bluu na kijani, sh. 8,000 viti vya rangi ya chungwa, sh. 15,000 kwa viti vya VIP C na B wakati VIP A itakuwa sh. 20,000.

Pia TFF inawaasa washabiki wa mpira wa miguu kuacha kununua tiketi mikononi mwa watu kwa vile wanaweza kuuziwa tiketi bandia. Tiketi zote zitauzwa katika vituo vinavyotangazwa katika magari maalumu, na uwanjani pia katika magari hayo.

Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa kuchukua washabiki 25,000 utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans na Mgambo Shooting kutoka Tanga. Ugumu wa mechi hiyo unatokana na ukweli kuwa timu zote mbili zinapigana kuepuka kurudi zilikotoka (daraja la kwanza).

Mgambo Shooting inayonolewa na Mohamed Kampira inashika nafasi ya tisa ikiwa na pointi 24 katika ligi hiyo yenye timu 14. Toto Africans ambayo iko nyumbani itaingia uwanjani ikiwa na pointi 14 katika nafasi ya 15 kwenye msimamo wa ligi.

Baada ya kulala 2-1 mbele ya Simba katika mechi iliyopita, Coastal Union itakuwa mgeni wa Mtibwa Sugar katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Manungu ulioko Turiani mkoani Morogoro.

Ligi hiyo itaendelea tena keshokutwa (Machi 17 mwaka huu) kwa mechi moja itakayozikutanisha JKT Ruvu na Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Azam Complex.

RAMBIRAMBI MSIBA WA OFISA HABARI CECAFA
Shrikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha aliyekuwa Ofisa Habari wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Finny Muyeshi kilichotokea juzi (Machi 13 mwaka huu) jijini Nairobi, Kenya baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Msiba huo ni mkubwa kwa wadau wa mpira wa miguu kwani Muyeshi aliitumikia CECAFA kwa muda mrefu, hasa katika kuhakikisha waandishi wa habari wanapata mazingira mazuri ya kufanyia kazi wakati wanaporipoti matukio mbalimbali ya Baraza hilo.

Alitoa mchango mkubwa katika eneo la habari za mpira wa miguu, tangu akiwa gazeti la East African Standard la Kenya akiwa mwandishi, na baadaye Mhariri wa Michezo kabla ya kujiunga na CECAFA, hivyo mchango wake tutaukumbuka daima.

TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Muyeshi, CECAFA, Shirikisho la Mpira wa Miguu Kenya (FKF) na tasnia ya habari kwa ujumla, na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Mungu aiweke roho ya marehemu Muyeshi mahali pema peponi. Amina

FDL KUKAMILISHA MSIMU WIKIENDI
Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu wa 2012/2013 unamalizika wikiendi hii huku timu za Mbeya City ya Mbeya, Ashanti United ya Dar es Salaam na Rhino Rangers ya Tabora zikiwa tayari zimepata tiketi ya kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao.

Kundi A mechi zote zitachezwa Jumapili (Machi 17 mwaka huu) ambapo Majimaji vs Mbeya City kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea, Kurugenzi vs Mkamba Rangers (Mafinga) na Burkina Faso vs JKT Mlale (Jamhuri, Morogoro).

Kesho (Machi 16 mwaka huu) katika kundi B itakuwa Green Warriors vs Polisi Dar (Karume, Dar es Salaam) na Ndanda vs Villa Squad (Nangwanda Sijaona, Mtwara). Keshokutwa (Machi 17 mwaka huu) ni Moro United vs Ashanti United (Karume, Dar es Salaam) na Tranist Camp vs Tessema (Mabatini, Mlandizi).

Kundi C ni kesho (Machi 16 mwaka huu) Polisi Tabora vs Pamba (Ali Hassan Mwinyi, Tabora). Keshokutwa (Machi 17 mwaka huu) ni Polisi Mara vs JKT Kanembwa (Karume, Musoma), Polisi Dodoma vs Mwadui (Jamhuri, Dodoma) na Rhino Rangers vs Morani (Ali Hassan Mwinyi, Tabora).

KILA LA KHERI AZAM KOMBE LA SHIRIKISHO
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linaitakia kila la kheri timu ya Azam kwenye mechi yake ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Barrack Y.C. II itakayochezwa Jumapili (Machi 17 mwaka huu) nchini Liberia.

Mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya kwanza itachezwa jijini Monravia na timu hizo kurudiana wiki mbili baadaye jijini Dar es Salaam. Ofisa Habari wa Azam yuko na timu hiyo Monrovia na anapatikana kwa namba +231888386655.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

MAAJABU YA SIMBA KWA MUFULIRA WANDERERS 1979

Droo Ligi ya Mabingwa Ulaya