in , , ,

Manchester United mbendembende

*Wachakazwa 4-1 na Manchester City
*Arsenal wafanya kweli, waongoza ligi

 
Wakati Arsenal wakishika usukani wa Ligi Kuu ya England, Manchester United wameoga kichapo cha mwaka, baada ya kuzama 4-1 kwa Manchester City.

Huo ulikuwa mtanange wa kwanza baina ya watani hao wa jadi msimu huu, ambapo wote wanafundishwa na makocha wapya.

Katika dimba la Etihad, Man U chini ya David Moyed hawakuwa na mshambuliaji wao tegemeo, Robin van Persie mwenye maumivu kidogo.

Man City chini ya Manuel Pellegrini walionekana kujiamini zaidi na kucheza kwa ari tangu mwanzo, na kuwaacha washabiki wakiwa na cheko la aina yake mwishoni, huku mmiliki, Sheikh Mansour aliyehudhuria akitosheka.

Mabao ya Man City yaliwekwa kimiani na Sergio Aguero, Yaya Toure, kabla ya Alvaro Negredo na Samir Nasri. Yalikuwa maumivu kwa mabingwa watetezi waliofutwa machozi na mkwaju wa adhabu ndogo wa Wayne Rooney.

Mshambuliaji huyo aliepuka kadi mapema baada ya rafu mbaya kisha kumpiga mchezaji wa Man City na mpira na nyingine kadhaa, lakini hadi mwisho alipata kadi ya njano tu.

Katika mechi ya awali, Arsenal walijipandisha kileleni mwa msimamo wa ligi kwa kuwapiga wagumu wa Stoke City kwa mabao 3-1.

Arsene Wenger alikuwa mwenye furaha, baada ya wachezaji wake kufanya kile alichowatuma, mabao yao yote matatu yakiandaliwa na mchezaji wake mpya, Mesut Ozil.

Waliopachika mabao wavuni ni Aaron Ramsey anayewika sana msimu huu na mabeki wake waliofunga kwa vichwa, nahodha Per Mertesacker na Bacary Sagna.

Stoke walionesha kujiandaa vyema kwani walisawazisha bao la kwanza kupitia kwa Mmarekani Geoff Cameron, lakini Arsenal hawakuwa tayari kukubaliana na sare.

Alimwanzisha kinda Sergre Gnabry badala ya Theo Walcott aliyegunduliwa kuwa na matatizo muda mfupi kabla ya mechi, na chaguo hilo la Kijerumani lililipa vyema kwa jinsi alivyojiamini na kumiliki mpira.

Katika mechi nyingine Tottenham Hotspur walipata bao la ‘jioni’ dhidi ya Cardiff City huko Wales na kuibuka na ushindi wa 1-0 ambao ni muhimu kwao.

Swansea nao waliwafunga Crystal Palace mabao 2-0 jijini London.
Kutokana na matokeo ya Jumapili hii na yale ya Jumamosi, Arsenal wanakali kiti cha uongozi, ambapo timu zote zimeshacheza mechi tano.

Arsenal wana pointi 12 sawa na Spurs, lakini wanawazidi wapinzani hao wa London Kaskazini kwa tofauti ya bao moja tu katika uwiano wao, wakifuatiwa na Man City na Chelsea wote wenye pointi 10 kama Liverpool.

Nafasi ya sita inashikwa na Everton kwa pointi zake tisa huku Southampton wakiwafuatia wakiwa na nane.

Man United msimu huu wamejikuta wakiwa nafasi ya nane wakifungana pointi na Swansea, Stoke, Hull na Newcastle.

Aston Villa wanafuatia katika nafasi ya 13 wakiwa na pointi sita, nyuma yao wanakuja West Bromwich Albion wenye tano sawa na West Ham na Cardiff.

Ukingoni mwa msimamo wanakuja Norwich wenye pointi nne sawa na Fulham, lakini nyuma yao wapo Crystal Palace wanaoshikilia pointi tatu na walipanda daraja msimu huu tu, na wanaozibeba timu zote ni Sunderland wenye pointi moja pekee.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Uchaguzi wa TFF: Nini sababu ya mizengwe?

Di Canio atupiwa virago Sunderland