in , ,

Leicester wazuiwa lakini …

 

*Chelsea wanapanda ‘mdogo mdogo’

*Mwamuzi wa akiba azimia uwanjani

Leicester wanaoongoza Ligi Kuu ya England (EPL) wamepunguzwa kasi kwa

kulazimishwa sare ya 2-2 na wagumu West Bromwich Albion, lakini kocha

wao, Claudio Ranieri amesema watapambana kuutafuta ubingwa.

Ilikuwa mechi nzuri, ambapo West Brom walitoka nyuma na kuhakikisha

wanapata pointi moja, tena wakiwa kwenye uwanja wa vinara hao wa muda

mrefu ambao hawakutarajiwa kabisa kufanya vyema, kwani walishatabiriwa

hata kushuka daraja.

Salomon Rondon alifanikiwa kumzidi maarifa Robert Huth na kuwapa West

Brom bao la kuongoza kabla ya Danny Drinkwater kusawaazisha kisha Andy

King akafunga bao lililodhaniwa lingekuwa la ushindi kwa Leicester.

Haikuwa hivyo, kwani West Brom walipata bao kupitia kwa Craig Gardner

aliyechonga vyema mpira wa adhabu ndogo.

Leicester waliendelea kutafuta ushindi, ambapo mara mbili mipira ya

wachezaji wake iligonga mtambaa wa panya. Wanabaki juu kwa tofauti ya

pointi tatu dhidi ya wanaowafuata, Tottenham Hotspur ambao wanaweza

kushika usukani wakipata ushindi Jumatano hii ugenini kwa West Ham.

Leicester wenye pointi 57 wamewaacha Arsenal umbali wa pointi sita, na

Jumatano hii Arsenal wanakipiga na Swansea. West Brom waliopoteza

mechi mbili tu kati ya 10 zilizopita wanashika nafasi ya 13 wakiwa na

pointi 36.

CHELSEA WANAPANDA ‘MDOGO MDOGO’

Diego Costa, akifunga bao...
Diego Costa, akifunga bao…

Chelsea wanaendelea kupata nafuu na sasa wamepanda hadi nafasi ya

nane, huku tishio la kushuka daraja chini ya Jose Mourinho likiondoka.

Wamefanya hivyo kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Norwich ugenini Carrow

Road chini ya bosi wa mpito, Guus Hiddink. Beki wa pembeni wa Chelsea,

Kenedy ndiye alifunga bao la kwanza kutoka umbali wa yadi 20 baada ya

kutiliwa mpira na Eden Hazard katika sekunde ya 39 tu, likiwa bao la

mapema zaidi katika EPL msimu huu.

Diego Costa alifunga bao la pili kuelekea nusu ya kwanza kumalizika,

katika kile kilichoonekana na wachambuzi wa mambo kwamba alikuwa

ameotea. Norwich ambao sasa wametupwa eneo la kushuka daraja hawakuwa

wazembe; walipambana ambapo mpira wa Cameron Jerome uligonga mwamba

kabla ya Nathan Redmond kufunga.

Norwich sasa wamepoteza mechi nane kati ya tisa zilizopita na kocha

wao, Alex Neil amelalamikia bao la Costa, akisema walau wangekwenda

sare. Wamevuna pointi moja tu kati ya 24 zilizokuwa mbele yao

kuzipigania.

MWAMUZI AZIMIA, MATOKEO MENGINE EPL

Kevin Friend, mwamuzi wa akiba akipatiwa matibabu uwanjani
Kevin Friend, mwamuzi wa akiba akipatiwa matibabu uwanjani

Katika matokeo mengine, Bournemouth wakicheza nyumbani waliwafunga

Southampton 2-0 katika mechi ambayo mwamuzi wa akiba, Kevin Friend

alizimia baada ya kujigonga kichwa kwenye chuma za eneo alikokuwa

amesimama kabla tu ya nusu ya kwanza kumalizika.

Mwamuzi huyo alitibiwa kwa muda uwanjani kabla ya kupelekwa hospitali

kwa uchunguzi na tiba zaidi. Mwamuzi wa kati, Mike Dean alisitisha kwa

muda mechi hiyo kabla ya kupuliza kipenga kuashiria kipindi cha

mapumziko na muda wa nyongeza haukuchezwa.

Kipindi cha pili kilichelewa kuanza kwa dakika tano, kwani mbadala wa

Friend alikuwa akitafutwa. Aliyechukua mikoba hiyo ni Dean Treleaven,

mwenye sifa zote za urefa lakini hajapata kuwa katika mechi ya ligi.

Ilikuwa siku nzuri kwa Bournemouth, kwani wamejiondoa kwenye eneo la

kushuka daraja kwa umbali wa point inane. Saints walipoteza nafasi

nzuri ya kufunga mapema, pale Charlie Austin alipobetua mpira kiupande

na kushindwa kufunga, hivyo wakabaki wakihangaika na watani wao hao

katika pwani ya kusini mwa England.

Bournemouth walifunga baada ya kipa Fraser Forster kuutema mpira wa

adhabu ndogo wa Matt Ritchie kisha Steve Cook akautumbukiza wavuni.

Benik Afobe aliwahakikishia ushindi The Cherries kwa kufunga akipokea

tena mpira wa adhabu ndogo wa Ritchie. Hii ni mara ya kwanza kwa

Bournemouth kuwafunga Saints katika ligi tangu 1958.

Sunderland na Crystal Palace walikwenda sare ya 2-2 na kuwafanya

Sunderland kuondoka kwenye eneo la kushuka daraja, japo kwa tofauti ya

mabao na Norwich na Newcastle, kwani wote wana pointi24 huku Aston

Villa wanaoshika mkia wakiwa na pointi 16.

Fabio Borini ndiye aliwanasua Sunderland kwenye matatizo baada ya

kusawazisha dakika ya 90. Dame N’Doye’s ndiye alianza kufunga bao kwa

Sunderland, lakini Connor Wickham akafunga mabao mawili katika kipindi

cha dakika mbili. Wangeshinda, Palace wangekuwa wamepata ushindi wa

kwanza katika mechi 11, lakini Borini aliyeingizwa kipindi cha pili na

kocha Sam Allardyce alifanya kweli kwa kucheka na nyavu, akionekana

kuwa ‘super sub’.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote
Tanzania Sports

Man City watwaa Kombe la Ligi

Tanzania Sports

KESSY ANAWAPA SIMBA FUNZO WANALOSTAHILI