in , ,

HOTUBA YA RAIS WA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU ALIPOZUNGUMZA NA WAHARIRI WA HABARI ZA MICHEZO JUMATATU MACHI 19,2018 KWENYE HOTEL YA SEASCAPE.

UTEKELEZAJI WA TFF KATIKA MAENEO MBALIMBALI

Ndugu Waandishi wa Habari,Sekretarieti ya TFF, Watanzania wote wanaotuangalia na kutusikiliza,mabibi na mabwana habari za asubuhi.

Naomba nianze kwa kumshukuru mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana mahali hapa siku ya leo tukiwa wazima wa Afya,Lakini pia nichukuwe nafasi hii kuishukuru Serikali ya awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Dr.Joseph Pombe Magufuli kwa ushirikiano mkubwa ninaoupata katika uendeshaji wa mpira wa miguu, nimekuwa karibu sana na Serikali kuhakikisha juhudi zetu za kuendeleza mpira zinafanikiwa kwa kasi kubwa sana na mafanikio ya ujio wa Rais wa FIFA ni kielelezo cha karibuni kuonyesha ushirikiano mkubwa tunaoupata toka kwa Serikali hasa Waziri mwenye dhamana ya michezo Mh.Dr,Harrison Mwakyembe na timu yake.

Lakini niwashukuru kwa nafasi ya kipekee ndugu zangu Waandishi wa Habari kwa kazi kubwa mnayoifanya kuhabarisha umma kuhusu habari za mpira wa miguu,Pia pongezi zenu kwa kazi nzuri mliyoifanya wakati wa ujio wa FIFA, mlifanya kazi kubwa sana kutangaza ziara ya Rais wa FIFA, mmetupa heshima kubwa sana.

Ndugu zangu, leo nitaongelea mambo makubwa mawili ili waTanzania wapate kufahamu kinachoendelea katika mchezo wa mpira wa miguu hapa nchini.

Moja nitaongelea kuhusu mambo ambayo tumeyafanya kwa kipindi cha miezi saba nilichokuwepo madarakani lakini la pili ni mambo yanayoendelea sasa hivi kwenye Shirikisho.

MAMBO AMBAYO TUMEYAFANYA KWA MIEZI SABA TOKA TUINGIE MADARAKANI

HALI NA SHUGHULI ZA TAASISI

Kwa Mazingatio ya Utekelezaji Makini na wa Maendeleo wa Shughuli za Taasisi Tulitambulisha Muelekeo na Dira ya TFF ambapo Kazi iliyo Mbele yetu ni Kuzitoa na Kuimarisha Utambuzi na Utekelezaji wake. Sasa ni wakati Tunajiandaa Kutoa baadhi ya Mipango yetu na kutoa Dira za Utekelezaji wake. Pamoja na Mipango hiyo Bado TFF tumekuwa Tukitekeleza Shughuli za Mpira katika Mgawanyiko wake na labda kwa kifupi kugusia Miongoni mwake.

Mashindano.

Tumeendesha mashindano mbalimbali kwa ufanisi mkubwa yakiwemo mashindano ya Azam Sports Federation Cup, Ligi ndogo ya Wanawake kwa ajili ya kupata timu za kupanda daraja,Ligi Kuu ya Wanawake hatua ya makundi na hatua ya nane bora inayoendelea,Mashindano ya soka la ufukweni kwa timu za vyuo vikuu,Mashindano ya kimataifa ya soka la ufukweni yajulikanayo COPA DAR ES SALAAM.

Azam Sports Federation cup;

Mashindano hayo kwa msimu huu 2017/18 tumeyaendesha kwa ufanisi na umakini mkubwa tofauti na huko nyuma kwa kuhakikisha upangaji wa ratiba umekuwa wa wazi usio na upendeleo wowote ule hivyo kupunguza malalamiko,jambo lingine tulihakikisha timu zote zinapata stahiki zao kwa wakati na kiwango kilichopangwa,kadiri tunavyoelekea hatua za mwisho wa mashindano tutahakikisha changamoto zote zilizojitokeza huko nyuma tunakabiliana nazo na kuzitatua ili kuhakikisha mashindano hayo yanaisha vizuri.

Ligi kuu ya Wanawake;

Mwaka huu tulianza kucheza Ligi ndogo ya Wanawake kutafuta timu za kupanda Ligi Kuu ya Wanawake katika vituo vya Dar es salaam na Dodoma,ikafuatiwa na Ligi ya Wanawake katika kituo cha Arusha na Dar es Salaam ili kupata Timu 8 za kucheza hatua ya Nane bora ya Ligi hiyo.

Katika hatua ya makundi, TFF ilizigharamia timu zote kwa asilimia 100 kuanzia malazi, usafiri, chakula, gharama za maadalizi ya timu na nauli ya kwenda na kurudi,ikiwa ni mara ya kwanza katika historia ya mpira wa miguu wa Wanawake kwa TFF kugharamia kwa kiwango hiki.

Katika hatua ya Nane bora ya Serengeti Lite Women Premier League vilabu vyote vilishapewa fedha zao kwa ajili ya hatua ya kwanza ambayo imesimama kupisha maandalizi ya timu ya Taifa ya Wanawake(Twiga Stars) ambayo inajiandaa na mashindano ya kufuzu michuano ya Afrika kwa Wanawake ambapo tayari timu ya Taifa ipo kambini ikijiandaa na mchezo huo dhidi ya Zambia.

Taasisi iliendesha kwa mafanikio makubwa mashindano ya soka la ufukweni (Copa Dar es Salaam) kwa kuzialika timu za Uganda, Malawi, Zanzibar na wenyeji Tanzania bara ambazo tulizigharamia malazi, chakula na usafiri wa ndani.

PROGRAMU ZA TIMU ZA TAIFA

Toka tumeingia madarakani, tumekuwa tunafanyia kazi program mbalimbali za maendeleo ya Timu za Taifa.

Taifa Stars

Tumekuwa tukiendelea na program mbalimbali za Timu ya Taifa za kuhakikisha inafuzu Fainali za kombe la mataifa Afrika 2019.

Kuhakikisha hili Taifa Stars ilicheza na Benin, Malawi, Botswana na wiki hii tunacheza na Algeria pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) katika kalenda ya mechi za kimataifa ya FIFA.

Ili kuongeza hamasa ya wachezaji tumeongeza posho ya ndani kwa asilimia 100 na asilimia 50 kwa posho za nje.

Kilimanjaro Stars

Timu yetu ya Tanzania bara ilishiriki mashindano ya CECAFA yaliyofanyika nchini Kenya mwezi Desemba 2017, mbali na kushiriki ili ichukuwe kombe sababu nyingine ilikuwa ni kuendelea kupata mechi nyingi za kimataifa.

Timu ilicheza dhidi ya Rwanda, Kenya, Zanzibar na Libya, Tunaamini kwa wachezaji vijana waliokuwa sehemu ya kikosi hicho imewajengea uwezo katika soka la kimataifa.

Timu za Taifa za Vijana

Katika eneo hili tumekuwa na mpango wa muda mrefu kuhakikisha vijana wa timu zetu za Taifa za miaka chini ya 23, 20, 17 na 13 zinakuwa na maandalizi bora na kwa kuanzia toka tuingie madarakani tumekuwa na kambi za timu za vijana kila mwezi kwa kuwakutanisha siku 14 za mazoezi na kuwatafutia mechi za kirafiki za kimataifa.

Timu ya U23

Timu ya Taifa chini ya miaka 23 ambayo ni kikosi cha pili cha timu ya Taifa kimeshaitwa kambini mara kadhaa na tumethibitisha kushiriki mashindano ya Olimpiki ambayo fainali zake zitafanyika nchini Japan, lengo ikiwa ni kuhakikisha tunawapatia vijana hawa mechi nyingi za kimataifa ili wawe tayari.

Timu ya Vijana U20

Timu ya Vijana U20 ambapo jana ilicheza na Morocco na Jumatano itacheza na Msumbiji, ikiwa ni maandalizi ya mechi dhidi ya timu ya vijana chini ya miaka 20 ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Congo(DRC) ikiwa ni mchezo wa kufuzu fainali za Vijana Afrika chini ya miaka 20.

Timu ya Vijana U16

Timu hii nayo imekuwa ikiingia kambini kila mwezi na hata sasa hivi ninavyozungumza na nyinyi, timu hii ipo kambini ikijiandaa kwa mashindano ya CECAFA na tunafanya jitihada za kuhakikisha inapata mechi mbili za kirafiki za kimataifa kabla haijaenda Burundi.

Timu hii ndiyo ambayo itashiriki fainali za Afrika chini ya miaka 17 zitakazofanyika hapa nchini mwaka 2019.

Baada ya kutoka Burundi itakuwa na program maalum kwa ajili ya kujiandaa kwa mashindano mengine ya kufuzu AFCON U17, 2019 ambayo yatafanyika nchini mwezi Agosti ambayo lengo ni kupata mwakilishi wa CECAFA na vijana wetu watashiriki kama wenyeji. TFF imeamua kushirikisha Timu yenye Umri mdogo zaidi kwa u17 bila ya kujali Matokeo zaidi ya Ujenzi wa timu kwa kuandaa timu moja katika matukio yote haya ili kuiweka tayari kwa Mashindano ya u17 ya 2019 mwakani ambapo vijana hawa ndio watakuwa rasmi u17

Timu ya Vijana ya U13

Timu ya Vijana ya U13 katika kutafuta namna ya Kuwaimarisha vijana hawa baada ya Utambuzi na Uteuzi wa timu imepata nafasi ya kushiriki mashindano ya kirafiki ya vijana chini ya miaka 13 yatakayofanyika nchini Ubelgiji mwezi Agosti 2018,Tayari orodha ya kwanza ya wachezaji 69 waliopatikana katika mashindano ya shule za msingi (UMITASHUMITA) ipo TFF na idara ya ufundi inaandaa utaratibu wa kuwaita pamoja na kupata michezo ya kirafiki dhidi ya Zanzibar kwa ajili ya kupata kikosi cha pamoja cha Tanzania.

Timu ya Taifa ya Wanawake U20

Tumeanza kuandaa kikosi cha Vijana cha timu ya taifa ya Wanawake U20 ili kuwa na kikosi bora cha Twiga Stars kilichoandaliwa kwa muda mrefu na tayari ilishacheza michuano ya kufuzu fainali za vijana za Afrika chini ya miaka 20 na kutolewa na Nigeria.

Baadhi ya wachezaji wa timu hii wamepandishwa kikosi cha wakubwa na sehemu kubwa wanacheza Ligi Kuu ya Wanawake kupitia vilabu mbalimbali.

Tutaendelea na utaratibu wa kuwaita kambini kila wakati kutakapokuwa na nafasi ili kuzidi kuimarisha kikosi.

Twiga Stars

Kikosi cha Twiga Stars kimeingia kambini kwaajili ya maandalizi ya mashindano ya kufuzu fainali za Africa kwa Wanawake zitakazofanyika nchini Ghana baadaye mwaka huu.

Twiga Stars inakabiliwa na mchezo dhidi ya Timu ya Taifa ya Zambia utakaochezwa Aprili 4,2018 Uwanja wa Taifa na marudiano kuwa Aprili 8,2018 nchini Zambia.

MAPATO NA MATUMIZI

MAPATO

Katika kipindi cha miezi Saba(7),Shirikisho limefanikiwa kukusanya kiasi cha Tzs 3,670,397,199.00 kutoka katika vyanzo vyake mbalimbali ambavyo ni pamoja na mapato kutoka kwa wadhamini Tzs 2,295,472,151 sawa na 62.5% ya mapato yote, makusanyo ya viingilio uwanjani Tzs 378,139,866 sawa na 10.3%. 27.2% ilitokana na Fedha kutoka CAF na FIFA.

MATUMIZI

Katika kipindi hiki Shirikisho lilitumia kiasi cha Tzs 3,752,001,171.00. Sehemu kubwa ya matumizi yalielekezwa kwenye usimamizi wa ligi mbalimbali pamoja na kuandaa timu za taifa ambapo jumla ya Tzs 2,409,150,732 sawa na 64% ya matumizi yote zilitumika.

Asilimia 36 ya Fedha zilizobaki ilitumika kulipia madeni ya Taasisi, Kulipa mishahara ya wafanyakazi, kusaidia mikoa katika maeneo ya miundo mbinu, kuwajengea uwezo wafanyakazi pamoja na kuendesha mafunzo mbalimbali.

Kama Rais wa TFF sijapokea HOJA wala USHAURI wala MAPENDEKEZO yoyote kutoka kwa Wajumbe wangu katika Ngazi zote kuhusiana na Matumizi ya Taasisi, Nasikitika kama kuna anayedai amehoji sijui wapi kwa kuwa kama Rais sijapokea hoja yoyote wala kuwasilishwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji iliyopita ambayo Taarifa ya Kamati ya Fedha iliwasilishwa nakupokelewa na kupitishwa na Kamati ya Utendaji.

MADENI

Katika kipindi hiki,Shirikisho lilianza zoezi la kutathmini madeni iliyoyarithi kutoka kwenye Uongozi uliopita, ambapo deni hilo linafikia Tzs 2,172,000,000 linalodaiwa na watoa huduma mbalimbali, wafanyakazi,wachezaji na makocha.

Asilimia kubwa ya deni hili lilitokana na malimbikizo ya deni la TRA, Workers Compensation Fund na NSSF ambalo lililimbikizwa kwa zaidi ya miaka miwili.

Shirikisho lilifanikiwa kulipa deni lote la michango ya wafanyakazi NSSF jumla ya Tzs 88,000,000 zilizokuwa hazijalipwa kipindi cha miaka miwili, na lilifanya majadiliano na Mamlaka ya Mapato Tanzania kuhusu ulipaji deni la kodi linalofikia Tzs 1,077,000,000, ambapo jumla ya Tzs 315,000,000 zimelipwa na kiasi kilichobaki tumekubaliana kitalipwa kwa awamu kadhaa mpaka deni lote litakapomalizika.

Pia shirikisho limefanikiwa kupunguza mishahara kwa wafanyakazi kutoka Tzs 85,063,092.00 mpaka kufikia 50,000,000.00 baada ya kupunguza idadi ya wafanyakazi kutoka 44 mpaka 21.

Baada ya kuingia madarakani tulifanya majadiliano na makocha wa timu za Taifa kuhusu uhalisia wa malipo yao na kufanikiwa kuokoa zaidi ya dola laki mbili(USD 200,000) kwenye mikataba yao na fedha zilizookolewa zitasaidia shughuli nyingine za mpira wa miguu.

UFUNDI

1. Kliniki iliyoendeshwa na Kocha PiaSundhage kutoka Sweden

2. Kozi ya ngazi ya awali ya makocha wa mpira wa miguu

ilifanyika katika mikoa ya Kigoma,Songwe, Lindi, Morogoro na Pwani

3. Kozi ya ngazi ya kati ya makocha wa mpira wa miguu

Ilifanyika katika mikoa ya Kigoma mara mbili, Manyara na Morogoro.

4.Grassroot & Live your goal project

Kozi hii ilifanyika katika mikoa ya Lindi ambapo washiriki walitoka katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Pia kozi nyingine ilifanyika katika mkoa wa Mbeya ambapo washiriki walikuwa ni kutoka katika mikoa ya Mbeya, Njombe, Katavi, Songwe na Rukwa

Aidha hii kozi ilifanyika Kigoma na kushirikisha washiriki wa mikoa ya Kigoma na Tabora.

5.Mafunzo ya awali ya Utawala mikoani

Kuna kozi ya utawala na masoko iliyofanyika Dar es Salaam ili kuwaongezea watu wa masoko uwezo wa kuwavutia wadhamini.

6.Mafunzo ya waamuzi

Mafunzo ya waamuzi wa FIFA na Waamuzi wa ngazi ya juu yalifanyika mara tatu jijini Dar es Salaam.

7. Kozi ya kupandisha daraja kwa Waamuzi

Kozi hii ilifanyika mara mbili katika mikoa ya Dar es Salaam na Mwanza.

8. Ziara za Mafunzo na kubadilishana uzoefu

Zilifanyika ziara mbalimbali za Waamuzi wetu za kubadilishana uzoefu katika nchi mbalimbali.


9. Mpango wa ugawaji wa vifaa vya vijana na mafunzo

Tulipoingia madarakani tulikuta uongozi uliopita wameshanunua mipira na imekaa stoo, katika kutekeleza azma ya maendeleo ya vijana ili tuwe na timu za Taifa imara Shirikisho limegawa mipira (100 kwa kila Mkoa) saizi 4 na 3 kwa Mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar, Mikoa imepewa vifaa vya kufundishia (cones and markers) ili vijana wapate fursa ya kuonesha na kuendeleza vipaji vyao kwa maslahi ya Mpira hapa nchini.


Uzinduzi wa zoezi hili ambalo linategemewa kuwa endelevu lilifanyika Uwanja wa Taifa Agosti 3, 2017.

Rais wa TFF aliwakabidhi wajumbe wa Kamati ya Utendaji kwa niaba ya Mikoa yao kwenye Kanda husika, Kwa upande wa Zanzibar Katibu Mkuu wa ZFA alikabidhiwa mipira hiyo kwa ajili ya Mikoa ya Zanzibar.


MASOKO NA HABARI

Tumeendelea kuongeza wadhamini katika maeneo mbalimbali ili kuhakikisha Taasisi inanufaika na bidhaa zake.Lakini pia tumeendelea kuimarisha idara ya habari kwa kuwanunulia nyezo za kufanyia kazi.

UTAWALA BORA

Katika kipindi hiki cha Miezi saba nimesimamia eneo hili kwa uadilifu mkubwa, Kamati zimekuwa zinakutana kabla ya vikao vya Kamati ya Utendaji ili kuhakikisha kila mmoja anashirikishwa.

Mfano, Wakati nilipokuwa mwenyekiti wa Kamati ya Fedha,kwa miaka 4 nilikaa kikao kimoja cha Kamati ya Fedha,Katika Utawala wangu aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ndani ya miezi saba ameitisha vikao visivyopungua vitano.

Nilimuagiza Kaimu Katibu Mkuu kuhakikisha kila Kamati ya Fedha inapohitaji kukutana ahakikishe inakutana na Mtendaji Mkuu amekuwa anatekeleza.

Na kwa sababu nafasi ya Makamu wa Raisi Kikatiba ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Mipango, basi hata mazungumzo ya Mkataba wa Udhamini wa Ligi Kuu msimu 2018/2019 yeye ndiye aliyekuwa anasimamia.

Nimekuwa nafanya hivi ili Taasisi iendeshwe kwa uwazi na kushirikisha kila mmoja,Na nimeendelea kusisitiza kuwa mapato ya matumizi ya Taasisi yatatolewa kwenye vyombo vya Habari ili yawe wazi kwa umma.

SEKRETARIETI YA TFF

Toka tuanze kuunda sekretarieti tumeajiri Wakurugenzi Watatu na Meneja mmoja na wote hawa waliajiriwa na Kamati ya Utendaji, Ofisi ya Katibu Mkuu haijawahi kuajiri mfanyakazi hata mmoja kufikia sasa.

Nafasi ambayo haijajazwa ni nafasi ya Katibu Mkuu ambako Ndugu Kidao Wilfred bado anakaimu.

Kwanza nikiri kazi nzuri inayofanywa na mtendaji mkuu aliyekuwepo katika kuhakikisha Taasisi inapiga hatua kwa kasi kila ninapokutana na watendaji wakuu wa FIFA, CAF na CECAFA wamekuwa hawasiti kunimwagia sifa kwa kuwa na sekretarieti mahiri iliyobadilika katika kufanyia kazi changamoto za Taasisi.

Raisi wa FIFA alisema anaona mabadiliko makubwa ya hatua tunazochukuwa, Lakini Katibu Mkuu wa FIFA alisema nina Sekretarieti ya Vijana wenye hali, nguvu na maono ya kuipeleka Taasisi mbele huo ndio ujumbe wao.

Nimeyasema haya kuwahakikishia nikiwa msimamizi wa sekretarieti, mambo yote ambayo Kaimu Katibu Mkuu amekuwa akiyafanya ni maelekezo yangu au utekelezaji wa maamuzi halali ya kamati ya Utendaji, Kwahiyo nichukuwe fursa hii kupongeza kasi ya sekretarieti katika kusimamia mambo mbalimbali.

AJIRA

Katika kipindi changu cha uongozi (Kamati ya Utendaji) kwa kushirikiana na ofisi ya Katibu Mkuu tumeweza kupunguza wafanyakazi kutoka Wafanyakazi 44 tuliowakuta wakati naingia madarakani hadi kufikia 21,Ni hatua kubwa na tunafanya upembuzi makini kabla hatujaanza kuajiri watu tuwe na mahitaji stahiki.

KATIBU MKUU

Kumekuwa na maneno mengi juu ya nafasi ya Katibu Mkuu wa Shirikisho, Ndugu zangu wakati naanza kazi niliona ni muhimu nafasi hii ikaimishwe kwa mtu anayelijua shirikisho vizuri na ambaye sina shaka na uwezo wake,Sifa zote hizi alikuwanazo KIDAO WILFRED na wajumbe wa Kamati ya utendaji chombo ambacho kinahusika nakupitisha kilibariki awe Kaimu Katibui MKuu.

Kutoka nje ya Ofisi na kukaimu hii siyo mara ya kwanza,wakati Ndugu Tenga anashinda Uraisi alimuomba Bi.Lina Kessy ambaye alikuwa mtumishi wa Serikali kuwa Mratibu wa Ofisi, nafasi iliyokuwa kama Mkuu wa sekretarieti wakati huo.

Hata wenzetu wa CAF, Rais ndiye anayepeleka jina bila kujali Mchakato utakavyokuwa kwa maana wanaweza wakatangaza au wasitangaze,na hata Katiba ya TFF inahitaji Rais wa TFF atoe mapendekezo ya Katibu Mkuu ili Kamati ya Utendaji ijadili, haya yanafanyika kwa sababu Rais kama msimamizi wa Sekretarieti anafanya kazi kwa karibu sana na Katibu Mkuu hivyo FIFA wanahitaji watu hawa wawe wanaoweza kufanya kazi kwa karibu sana,ndipo Rais wa TFF anapopewa kipaumbele cha mtu wa kufanya naye kazi kwakuwa ndio nguzo ya Taasisi kwakuwa Rais ndio mkuu wa Taasisi na Katibu Mkuu ndio mkuu wa Sekretarieti.

Lakini pamoja na yote hayo bado nilikuwa napeleka ajenda ya Ajira kwenye Kamati ya Utendaji ili kushauriana njia bora ya kupata Katibu Mkuu kwa maslahi mapana ya Mpira wa Miguu na siyo mtu.

Niwahakikishie kikao kijacho cha kamati ya Utendaji kitaamua njia sahihi ya kupata Katibu Mkuu na tutahakikisha tunakuwa na Katibu Mkuu ndani ya muda mfupi ujao.

Mipango Mbalimbali

Tumekuwa katika Ujenzi wa Mipango Mbalimbali kama nilivyoainisha kwenye Ilani yangu ambapo Katibu Mkuu amekuwa Kiungo muhimu katika kunisaidia kwenye Ujenzi wa Mipango yangu hiyo lakini kwa bahati Mbaya Kaimu Katibu Mkuu Kidao amekuwa kwenye wakati mgumu kutokana na kuandamwa na Maneno na Vitendo vinavyolenga na kufanikisha kumkwamisha na kumkosesha mazingira bora na rahisi ya kufanyia kazi zake na hivyo imekuwa ni atahri kwa TFF kwa Baadhi ya Mipango yake kuwa inakwama kutoka Mpaka sasa na hiyo ni athari kwa Mpira wetu kwa Ujumla.

Ndugu zangu jambo la pili ambalo nimeona niligusie ni jinsi vyombo vya maamuzi vya TFF vinavyofanya kazi,

Ndugu waandishi, TFF inafanya kazi kwa mujibu wa Katiba yake ya mwaka 2013 na kufanyiwa marekebisho mwaka 2015. Katiba hii inataja Kamati ya Utendaji itaundwa na Wajumbe wafuatao;

1. Rais

2. Makamu wa Rais

3. Wajumbe 13 kutoka kanda zilizotajwa ibara 32 ya katiba ambazo ni Kanda namba 1-Kagera na Geita

Kanda namba 2- Mara na Mwanza

Kanda namba 3- Shinyanga na Simiyu

Kanda namba 4- Arusha na Manyara

Kanda namba 5- Kigoma na Tabora

Kanda namba 6- Katavi na Rukwa

Kanda namba 7- Mbeya, Iringa na Songwe

Kanda namba 8- Njombe na Ruvuma

Kanda namba 9- Lindi na Mtwara

Kmada namba 10- Dodoma na Singida

Kanda namba 11- Pwani na Morogoro

Kanda namba 12- Kilimanjaro na Tanga

Kanda namba 13- Dar es Salaam

4. Wajumbe wawili wanowakilisha vilabu vya Ligi Kuu

5.Mwenyekiti wa Chama cha Soka ya Wanawake.

6. Mwenyekiti wa Kamati ya Tiba

7. Wajumbe wawili wa kuteuliwa na Rais wa TFF.

Rais wa TFF amepewa nafasi za kuteua wajumbe wawili wa kamati ya Utendaji ili kumsaidia kufanya kazi na watu ambao wanajua muelekeo wake lakini ambao anaamini watamsaidia kwenye maeneo mbalimbali katika Taasisi.

Kamati ya Utendaji inafanya kazi na vyombo mbalimbali ambavyo ni Kamati ndogondogo, Bodi ya Ligi na Kamati za Kisheria pamoja na Kamati za Uchaguzi.

Kamati Ndogo ndogo;

Fedha na Mipango
Mashindano(Kamati ya Tuzo na Soka la Ufukweni)
Ufundi na Maendeleo
Vijana
Wanawake
Waamuzi
Katiba, Sheria, na Hadhi za wachezaji.
Tiba
Ukaguzi (ambayo yenyewe ni kama Kamati huru)

Kamati za Kisheria;
Nidhamu
Rufani ya Nidhamu
Maadili
Rufani ya Maadili

Kamati za Uchaguzi;

Uchaguzi
Rufani ya Uchaguzi

Ufanyaji wa kazi wa Kamati hizi umeelezewa katika Katiba ya TFF kwa maana Kamti za Kisheria zinajitegemea huwa haziingiliwi kwenye maamuzi yake.Ingawa vikao vyake vyote huwa vinaratibiwa na ofisi ya Katibu Mkuu.

Kwahiyo maamuzi ya Kamati hizi huwa ni ya kujitegemea hivyo watu wote ambao wamekuwa wanahukumiwa na Kamati hizi ni vyema wakawa wanajua utaratibu wa Kamati zinavyofanya kazi.Na mimi binafsi nimeendelea kuheshimu Kamati zifanye kazi bila kuingiliwa na mtu yoyote vile.

Ndiyo maana wakati nachaguliwa niliahidi kusimamia Taasisi kwa uadilifu mkubwa bila kumuonea aibu mtu yeyote, wala kumuogopa mtu na hii ni katika kuunga mkono juhudi za Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kupambana na uchafu wa aina zote katika serikali,Nami nimeamua kusafisha Taasisi kama nilivyoahidi wakati wa Kampeni za uchaguzi ulioniweka madarakani,niseme wazi hakuna mtu asiye muadilifu atabaki katika mpira,Na nimpongeze Kaimu Katibu Mkuu wangu kwa kusimamia kwa ujasiri mkubwa usimamiaji wa maagizo yote halali ya Kamati mbalimbali,Amekuwa anasimamia bila uoga bila kujali anavyosakamwa kwangu linanipa faraja sana.

The Tanzania Football Federation (TFF) President Wallace Karia
The Tanzania Football Federation (TFF) President Wallace Karia

Tumekuwa tunachukuwa hatua katika kila eneo tumeshaanza kuchukuwa hatua kwa wizi wa Mapato ya milangoni, kuna viongozi wamefungiwa,hatukuishia hapo tayari viongozi walioghushi leseni za usajili wamefungiwa,Hiyo yote ikiwa ni kuonesha sina masihara hata kidogo kwenye kuhakikisha mpira unakuwa sehemu ya watu waadilifu.

FIFA walituma Timu ya Uchunguzi(Investigation Team) kuangalia yale yote yaliyofanyika toka mwaka 2013 mpaka mwaka 2017,Timu ilikaa nchini kwa takribani wiki mbili ikifanya kazi kwa karibu na Ofisi ya Katibu Mkuu,Yaliyogundulika yameacha doa kubwa na walitoa Ripoti na Maelekezo ya mambo ya kuyafanyia kazi na ya kuchukulia hatua.

Masharti yote haya yaliambatana na kuzuiwa kwa fedha zetu za miradi nia na wenzetu wachache, Lakini tumekosa pesa zinazoitwa Operation Cost ikiwa ni shinikizo la Dola Milioni Tatu ambazo tulipaswa kulipwa toka mwaka 2015-2018.

Karibia nchi zote Duniani zimenufaika kwa kupata pesa hizi, isipokuwa Tanza kuhakikisha tunatekeleza masharti ya FIFA, Hivyo tulipopata ripoti tumeamua kutekeleza kwa asilimia mia moja maagizo yote ya FIFA. Haya yanayotokea ni Miongoni mwa Matokeo ya Utekelezaji wa Taarifa za Wakaguzi wa TFF na Wakaguzi na Timu ya Uchunguzi kutoka FIFA. Jambo hili limepitia Hatua stahiki kwa Mujibu wa Taratibu zinazohusiana na Taarifa za kiUkaguzi na wahusika wameshirikishwa ipasavyo na Utetezi wao walipeleka kwenye Kamati husika ya Ukaguzi miezi iliyopita baada ya kutakiwa kufanya hivyo kwa mujibu wa taratibu.

Niseme tu unaposafisha Taasisi kuna gharama zake TFF inahitaji Kuungwa Mkono zaidi kwa Hatua Madhubuti inazochukua za Kujisafisha na Kusonga Mbele.

Katika VITA hii ya Kupambana na Udhalimu kwenye Mpira wetu Hatutarudi Nyuma, Tutapambana bila hofu wala woga almuradi Hakuna dhulma wala Uonevu wala Upendeleo kwa yeyote. Na Nitoe wito kama kuna Kiongozi au Mdau yoyote anayejua ana Pesa za TFF kinyume cha Utaratibu Natoa WITO Ajisalimishe Mwenyewe.

Ahsanteni kwa kunisikiliza naamini mtaniunga mkono ili kuusogeza mbele Mpira wa Tanzania.

Mwisho niwakumbushe TFF inaendelea na maandaalizi ya Matayarisho wa AFCON U 17,2019 .Timu ya ukaguzi ya CAF itakuja mwezi wa Tano, tumekuwa tunalifanyia kazi kwa ukaribu na serikali kuhakikisha changamoto za viwanja vitavyochezea mashindano pamoja na viwanja vya mazoezi vinakuwa tayari kwa wakati.Tutaendelea kulitolea ufafanuzi kila wakati.

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote
Tanzania Sports

VIATU VYA SCOTT VIMEFICHA PESA ZA POGBA

Tanzania Sports

SALAH ANAWEZA KUMSHINDA MESSI, LAKINI NI ZIADA YA MAHITAJI NDANI YA BARCELONA