in , ,

Hongera Abdulhalim Humud: Jomo Cosmos isiwe mwisho wa safari..

HABARI kwamba kiungo mwenye kipaji kikubwa cha soka nchini Abdulhalim Humud wa Azam amefuzu majaribio kwenye klabu kubwa ya soka ya Jomo Cosmos ya Afrika Kusini ni habari ya kusisimua, ya kufurahisha lakini si ya kushangaza.

Inasisimua kwamba Humud anaingia kwenye orodha ya majina makubwa katika soka ya Afrika ya kina Tico-Tico wa Msumbiji, Mark Fish, Phil Masinga, Aaron Mokoena, Mark Williams wa Afrika Kusini, Bruce Globbelaar wa Zimbabwe, Chris na Felix Katongo wa Zambia na wengine wengi wa hadhi zao katika orodha ya wachezaji watakaowahi kuichezea timu hiyo ya Afrika Kusini inayopigana kurudi kwenye ligi kuu (Premier Soccer League) ya nchi hiyo baada ya kushuka daraja toka daraja hilo hadi la kwanza (National First Division) kwenye msimu wa 2009-10.

Hii ni habari ya kufurahisha kutokana na ukweli kwamba Humud ameshinda majaribio ya kuchezea timu inayoweka mikakati mizito kurudi ligi kuu. Ni wazi kufanikisha mikakati hiyo lazima timu hiyo inatafuta vifaa vya uhakika na si vya ubabaishaji ili kufikia lengo lake. Kwa msingi huo, ni wazi Humud ni kifaa kweli kweli.

Ukweli ni kwamba klabu yoyote yenye shinikizo fulani kubwa kama juhudi za kupanda daraja, kuchukua ubingwa iliyoupoteza, kutetea ubingwa iliyo nao, kutohangaika kutoshuka daraja kama msimu uliotangulia na mengineyo, hutafuta wachezaji wa nguvu ili kufanikisha lengo husika. Kwa hiyo Mtanzania Humud ni kifaa cha ukweli.

Habari hii haishangazi kwani Humud anaujua mpira kweli kweli. Ni matatizo kadhaa, hasa majeraha ya mara kwa mara, ndiyo yamemuondoa kwenye timu ya taifa na kupunguza uchezeshwaji wake kwenye timu yake ya Azam. Huyu ni mchezaji ambaye watangazaji wa kituo cha runinga za michezo cha Supersport cha Afrika ya Kusini walimshangaa, mara kadhaa waliposhughulika na uonyeshaji wa mechi zetu toka Tanzania, kwa nini hachezi soka ya kulipwa Ulaya au kwingineko kwenye soka kubwa.

Aidha, wachezaji na makocha wa timu maarufu za taifa za bara hili tulizocheza nazo,Humud akicheza,kama Cameroon, Ivory Coast na Misri walimsifu sana wakisema mchezaji huyo, mzaliwa wa Zanzibar, kucheza ligi ya Tanzania si sahihi kwa kipaji chake cha hali ya juu.

Anachopaswa kufanya Mtanzania mwenzetu Humud kwenye ajira yake mpya ni kutopuuza mazoezi, kufanya mazoezi kwa bidii, kujituma, kwa kuzingatia maelekezo na kushiriki mazoezi hayo kila alipohitajika kufanya hivyo na kuacha visingizio. Akipata nafasi ya kupangwa, acheze kwa juhudi na maarifa kwa kufuata maelekezo na kuingiza ubunifu wake wa kuleta manufaa inapojitokeza hali isiyotarajiwa uwanjani. Awe na nidhamu ya hali ya juu wakati wote, heshima na upendo kwa wote na ajiepushe na homa ya nyumbani (home sickness).

Malengo yake yawe kujitahidi ili afike mbali zaidi ya Jomo Cosmos katika soka kwani bado ana miaka yakutosha ya kuucheza mchezo huo ikizingatiwa kuwa amezaliwa tarehe 12/03/1987 na hivyo kuwa na umri wa miaka 26 tu. Achagizwe kwa hilo na historia ya baadhi ya waliomtangulia kuchezea timu hiyo. Kipa Globbelaar alichezea Liverpool ya Uingereza. Mark Fish alifika Lazio ya Italy kisha Bolton Wanderers, Charlton Athletic na Ipswich Town za Uingereza.

Aaron Mokoena, aliyechezea pia timu ya vijana ya Bayer Leverkusen ya Ujerumani kisha timu za wakubwa za Ajax ya Uholanzi, Blackburn Rovers na Portsmouth za Uingereza, alianzia kwenye timu ya vijana ya Jomo Cosmos. Mark Williams alichezea Wolverhampton Wanderers ya Uingereza.

Hii ni mifano michache tu ambapo kama Humud atazingatia kuwa na nidhamu na masuala ya kutopuuza mazoezi, kufanya mazoezi kwa bidii, kujituma, kwa kuzingatia maelekezo na kucheza kwa juhudi na maarifa, naye atafika huko kwani mpira anaujua na sasa atakuwa ndani ya klabu inayoendeshwa kitaalam kama taasisi. Hata Azam yake inajitahidi kuwa hivyo lakini inaangushwa na Utanzania unaoizunguka.

Inaleta raha sana wachezaji wa kulipwa wanavyoongezeka kama hivi. Tuna Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu walio wafumania nyavu matata sana. Sasa tunampata kiungo wa nguvu Abdulhalim Humud. Kwa changamoto hii ya Humud, ni wazi timu yetu ya Taifa itajaza wachezaji wa kulipwa wa nafasi zote hivi karibuni.

Abdulhalim Humud timiza wajibu wako vizuri Afrika ya Kusini lakini ukijiwekea msimamo kuwa hapo uko njiani tu kuelekea Ulaya. Uwezo unao, sababu ipo kwa hiyo jenga nia. Uwezo unao kwa sababu soka unaijua kwa hiyo safari ya Ulaya inategemea uamuzi wako wa kujituma na kuwa na nidhamu huko ugenini. Kila la heri Mtanzania mwenzetu Abdulhalim Humud Mohammed.

20130404-182921.jpg

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

TFF YAZINDUA MPANGO WA MAENDELEO 2013-2016

Chelsea wang’aa Europa