in , , , ,

Crystal Palace watua Ligi Kuu


*Wanaungana na Cardiff na Hull EPL
*Benitez ateuliwa kocha mkuu Napoli

Hatimaye kitendawili cha timu zitakazocheza Ligi Kuu ya England (EPL) msimu ujao kimeteguliwa katika uwanja wa Wembley, baada ya Crystal Palace kutwaa nafasi ya tatu na ya mwisho katika mchezo mkali dhidi ya Watford.
Palace wanaungana na klabu nyingine mbili zilizokuwa nayo ngazi ya pili ya ligi – Championship – Cardiff City na Hull City kuingia kwenye ligi kubwa zaidi nchini Uingereza na maarufu zaidi ya zote duniani, ambapo hatua hiyo inathamanishwa na pauni milioni 120, kwa uchache.
Palace walikwenda hadi muda wa ziada kupata ushindi wao kwa mkwaju mmoja wa penati, baada ya Wilfred Zaha kuchezewa vibaya kwenye eneo la penati, ambapo mkongwe Kevin Philips alikwamisha wavuni shuti kali, na kumwacha nahodha wa Watford na kipa wa zamani wa Arsenal, Manuel Almunia akiukosa, japo aliuendea juu kona ya kulia.
Zaha anaondoka kwenda Manchester United msimu ujao, na amechangia kwa kiasi kikubwa kuwapandisha daraja Palace, wakati Philips naye anasema anapumzika soka, na atafikiria baadaye kipi cha kufanya, kama kucheza tena au kuwa kocha, maana sasa ana umri wa miaka 39.
Kocha Ian Holloway alionesha furaha isiyo ya kawaida kwa ushindi huo, akionekana mtu muhimu aliyeifufua, baada ya kupoteza makali yake, na miaka michache iliyopita ilikaribia kusambaratika na kushuka daraja 2009/10, baada ya kufilisika.
Kocha wa Watford, mchezaji mahiri wa zamani, Giafranco Zolla alijawa masikitiko, pamoja na mchezaji Marco Casseti aliyesababisha penati kwa rafu ambayo haikuwa ya lazima, na laiti wangeendeleza kukaba vyema, mchezo ungeenda hadi kwenye matuta. Watford nusura wasawazishe dakika za lala salama, lakini mpira wa kichwa wa Joel Ward uliokolewa kwenye mstari na Fernando Forestieri.
Palace wanaweka rekodi kuwa klabu ya kwanza kupanda EPL kwa mara tano, na safari hii Holloway anasema watagangalama na kubaki, si kama mara zilizopita. Mara ya mwisho walishuka daraja mwaka 2005.

RAFA BENITEZ KAMA MFALME ITALIA

20130527-224007.jpg

Kocha wa Muda wa Chelsea, Rafael Benitez Maudes ameteuliwa kuwa kocha mkuu wa Napoli ya Italia. Rafa Benitez (53) alikuwa akisubiri kazi mpya, kwani aliyokuwa nayo ilikuwa ya muda hadi mwisho wa msimu huu, na huko Italia anachukua nafasi ya Walter Mazzurri aliyefukuzwa na kujiunga na wapinzani wa jadi wa Napoli kwenye Serie A, Inter Milan.
Rais wa Napoli iliyoshika nafasi ya pili msimu huu, Aurelio De Laurentiis amemwelezea Benitez kuwa ni mtu maarufu mwenye uzoefu wa kimataifa na kwamba ni kiongozi mzuri ambaye atawawezesha Napoli kutwa mataji msimu ujao.
Rais huyo hivi majuzi alikuwa akisherehekea siku yake ya kuzaliwa kwenye hafla kubwa, akasema kwamba amepata zawadi ya pekee kwa siku hiyo, na kwamba ilikuwa kocha nguli, Benitez, japokuwa baadaye alikanusha kumtaja jina, akisema bado ameajiriwa Chelsea na anapenda kufuata sheria na kanuni.
Benitez aliyepata umaarufu zaidi kwa miaka mingi aliyowaongoza Liverpool, anamaliza kazi Chelsea kwa kuwapatia Kombe la Europa na nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi, hivyo kufuzu kushiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya mwakani.
Benitez pia aliwafikisha Chelsea kwenye Kombe la Dunia la Klabu la Fifa walikofungwa na Corithians ya Brazil na kabla ya hapo aliwaongoza Valencia ya Hispania kutwaa taji la La Liga (2001-02, 2003-04); Kombe la Uefa (2003-04); Liverpool Kombe la FA (2005-06); Ngao ya Jamii (2006); Kombe la Ulaya (2004-05); Uefa Super Cup (2005). Pia aliwaongoza Inter Milan kutwaa Supercoppa Italiana (2010) na Kombe la Dunia la Klabu la Fifa mwaka 2010.
Pamoja na mafanikio hayo, hakuwa akipendwa na washabiki wa Chelsea, waliozoea kumzomea na kumshikia mabango ya kumtaka aondoke, wakionesha wazi kuchukizwa na jinsi mtangulizi wake, Roberto Di Matteo alivyofukuzwa kazi. Inatarajiwa kwamba Jose Mourinho atajiunga Chelsea baada ya kuaga Real Madrid rasmi.

 

Enhanced by Zemanta

Report

Written by Israel Saria

For the last 20 years I have been working as a football pundit. This experience has provided me with a very useful insight into football and the opportunity to carry out extensive research into the game including its players, the stadiums, the rules and tactics and I have also been grateful to meet a wide range of people connected to football in the UK, Tanzania, Germany .....

What do you think?

71 Points
Upvote Downvote

Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Loading…

0

Kocha Bayern ataka kibarua cha Mourinho

TAIFA STARS YAANZA KUJINOA ADDIS ABABA